Sehemu Ya Kwanza: Wajibu Wa Wanawake
Madhumuni ya ndoa
Ndoa ni haja ya kawaida kwa kila mwanadamu. Inayo manufaa mengi na mazuri, baadhi ya hayo manufaa mengi na mazuri yaliyo muhimu ni haya: Ujengaji wa familia ambayo kwayo mtu anaweza kupata usalama na utulivu wa akili. Mtu ambaye hakuoa au kuolewa hufanana na ndege asiye na kiota. Ndoa hutoa huduma ya hifadhi kwa kila mtu anayehisi amepotea kwenye maisha yasiyo na mpango; mtu anaweza kupata mwenzi wa maisha ambaye anaweza kushirikiana naye katika furaha na huzuni.
Matamanio ya kawaida ya kijinsia yana nguvu na yenye maana. Kila mtu anatakiwa kuwa na mwenzi kwa lengo la kujitosheleza kijinsia kwenye mazingira yaliyo salama na tulivu. Kila mtu anapaswa kufaidi raha mustarehe ya kijinsia katika namna iliyo sahihi na inayostahiki. Wale wanao jiepusha na ndoa mara kwa mara husumbuliwa na maradhi ya kimwili na kisaikolojia.
Maradhi hayo na matatizo fulani ya jamii ni matokeo ya moja kwa moja ya vijana kujiepusha na ndoa.
Uzazi: Kupitia kwenye ndoa, binadamu wanaendelea kuzaana. Watoto ni matokeo ya ndoa na ni vipengele muhimu katika kuimarisha misingi ya familia na halikadhalika kama chanzo cha furaha kwa wazazi wao. Msisimko mkubwa sana umebainishwa kwenye Qur’ani Tukufu na Hadith kuhusu ndoa na kupata watoto. Mwenyezi Mungu Mweza wa yote anasema kwenye Qur’ani Tukufu:
وَمِنْ آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ {21}
“Na katika Ishara zake ni kuwa Amekuumbieni wenza kutokana na nafsi zenu...” (Quran 30:21).
Mtume (s.aw) alisema: “Hapana muundo ulio bora zaidi ulio asisiwa katika Uislamu kuliko ndoa.”
Imam Ali (a.s) alisema: “Shiriki katika ndoa; kwa sababu hii ni Suna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w).”
Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alisema: “Yeyote anayefuata Suna yangu lazima aowe na kuzaa watoto ambao ni matokeo ya ndoa na kuongeza umma wa Waislamu ili kwamba katika Siku ya Ufufuo nitakabiliana na umma wa mataifa mengine nikiwa na idadi kubwa ya umma wangu.”
Imam Ridha (a.s) alisema: “Mafanikio makubwa sana ya mtu ni kuoa mke mwaminifu, ambaye kila amuonapo anafurahi na hulinda mali yake na heshima yake mwenyewe wakati akiwa hayupo.”
Kilichozungumziwa katika sura hii kwa upande wa ndoa ni mambo yahusuyo dunia na maumbile tu ambayo pia wanyama wanayo; manufaa ya urafiki na kuzaana.
Kama ilivyo madhumuni ya kweli ya ndoa kwa jamii ya binadamu ni ya aina tofauti. Binadamu hakukusudiwa kuingia katika dunia hii kwa sababu ya kula, kunywa, kulala, kutafuta starehe au kuendekeza ashiki na halafu kufa na kuharibika. Hadhi ya mwanadamu ni ya juu zaidi kuliko matendo kama hayo. Wanadamu wanakusudiwa kujifunza wenyewe na roho zao katika kupata ujuzi, kufanya matendo mema na kuwa na tabia njema. Binadamu amekusudiwa kuchukua hatua kwenye njia iliyonyooka ili apate ukaribu wa Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.
Mwanadamu ni kiumbe ambacho kinaweza kusafisha roho yake kwa kuepuka matendo maovu na kujizoeza kuwa na tabia njema hufikia kiwango cha hadhi ya juu sana ambayo kwamba hata malaika hawezi kuipata.
Binadamu ni kiumbe ambacho ni cha milele. Amekuja hapa duniani ili kwa mwongozo wa manabii na utekelezaji wa utaratibu uliowekwa na dini ya Uislamu, aweze kupata furaha yake hapa duniani na Peponi, ili kwamba aweze kuishi maisha ya amani katika dunia ijayo daima milele.
Kwa hiyo, madhumuni ya ndoa lazima yatafutwe katika muktadha huu wa kiroho. Lengo la ndoa kwa mtu wa dini lazima iwe ni njia ya kuepusha matendo maovu na kutakasa roho kutokana na madhambi. Lazima iwe ni njia ya kupata ukaribu kwa Mwenyezi Mungu Mweza wa yote. Ni katika muktadha huu kwamba mwenza anayefaa na mwema huchukua jukumu muhimu.
Waumini wawili wanapounda familia kupitia katika ndoa, uhusiano wao wa kijinsia utawanufaisha katika kuimarisha mapenzi na wema wao, kwa wanandoa wa aina hiyo hapangekuwepo na hatari ya kutishia potovu wa kijinsia, mazoea mbaya au matendo ya haramu. Mtume (s.a.w) wa Uislamu na Maimamu wote (a.s) wamesisitiza sana kuhusu taasisi hii ya ndoa.
Mtume (s.a.w.w) alisema: “Yeyote anayeoa amelinda nusu ya dini yake.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Rakaa mbili za Swala ya mtu aliyeoa ni zaidi ya rakaa sabini za Swala ya mtu ambaye hakuoa.”
Mumini mchamungu na mwenzi mpatanifu hutekeleza jukumu la maana sana katika kupata na maisha ya kuheshimika na kuaminika.
Kwa kweli kuwa na mwenzi wa aina hii ni kipengele muhimu kwa mtu anapotaka kuepuka matendo maovu na kuwezesha msimamo wa mtu katika kutekeleza matendo ya wajibu ya ibada.
Wanandoa wachamungu, si tu kwamba hawatakutana na vikwazo vyovyote katika kufanikisha malengo ya kidini, bali watakuwa chanzo cha kutiana moyo wenyewe kwa wenyewe.
Je, inawezekana kwa mtu muumini wa Mwenyezi Mungu kupigana kwa utukufu katika njia Yake bila ya uthibitisho wa mke wake? Je, inawezekana mtu yeyote mchamungu kupata riziki yake kihalali, kwa kuzingatia vipengele vyote vya kidini, kulipa sadaka iliyoamriwa kisheria ili kuepuka ubadhirifu, na kutumia katika kutoa msaada bila ya idhini ya mkewe?
Mchamungu kila mara angemlingania mwenzi wake kwenye wema, kama vile ambavyo mtu mpotovu angemshawishi mwenzi wake kuwa mpotovu.
Halafu ni jambo la maana kwamba kwenye Uislamu wanamume na wanawake ambao wanataka kuoa au kuolewa wanashauriwa kuangalia usafi na tabia njema za wale wanaotaka kuwa wenzi wao katika maisha ya ndoa, kama masharti ya muhimu.
Mtume (s.a.w.w) alisema: “Kama ingetokea mimi nimpe mtu Mwislamu mazuri ya dunia na akhera, ningemjalia moyo wa unyenyekevu, ulimi ambao ungetamka sifa Zake mfululizo, mwili wenye kuvumilia maafa yote, na ningempa mwenza katika ndoa mchamungu ambaye akimuona tu anafurahi, na analinda mali yake na heshima yake mwenyewe asipokuwepo.”
Mtu mmoja alikwenda kwa Mtume na akasema: “Ninaye mke ambaye hunikaribisha nyumbani kila ninaporudi na hunisindikiza hadi mlangoni ninapoondoka.
Anaponiona mimi nimehuzunika na sina furaha, kwa kuniliwaza na husema: ‘Kama unafikiria kuhusu riziki, basi usikate tamaa, kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye anayetoa riziki na kama unafikiria maisha yajayo, basi Mwenyezi Mungu na akuongeze akili yako na jitihada zako.’ Halafu Mtume (s.a.w.w) akasema; “Hakika Mwenyezi Mungu anao watendaji na wawakilishi hapa duniani na mke ni mmojawapo. Mwanamke wa namna hii atazawadiwa thawabu nusu ya mtu aliyejitolea mhanga.”
Imam Ali (a.s) alikuwa anafikiria haya haya aliposema kuhusu Hadhrat Zahra (a.s). Alisema kwamba mkewe alikuwa msaada mkubwa katika kumcha Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.
Historia inatuambia kwamba, siku moja kipindi kifupi baada ya harusi ya imam Ali (a.s) na Hadhrat Zahra (a.s), Mtume (s.a.w.w) alikwenda kuwapongeza nyumbani kwao na kujua hali yao. Alimuuliza Imam Ali (a.s): “Unamuonaje mkeo?” Imam akajibu; “Nilimuona Zahra kama msaada mzuri sana katika kumuabudu Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.
Halafu Mtume aliuliza swali hilo hilo kwa Zahra (a.s) naye alijibu: “Mwenzangu ni mume mzuri sana.”
Katika sentensi moja, Imam Ali (a.s) alimtambulisha mwanamke bora katika Uislamu na akaelezea madhumuni makuu ya ndoa.
Kuishi Na Mume
Kazi ya mke ni kumtunza na kumlea mume. Si kazi rahisi. Wanawake hao ambao hawatambui sifa hii ya wajibu wao, wataona vigumu katika kutimiza kazi hii.
Ni kazi ya mwanamke ambaye anatambua kwamba kazi hii inahitaji kiwango fulani cha busara, mtindo na ustadi. Kwa mwanamke kuwa mke aliyefuzu, lazima auteke moyo wa mume wake na kuwa chanzo cha furaha kwake.
Lazima amtie moyo katika kutenda matendo mema na kumshawishi asifanye matendo maovu. Lazima pia mke achukue hatua za kutosha kutunza afya yake na ustawi wake. Matokeo ya bidii yake yanaelekezwa katika kumfanya mume awe mwema na anaye heshimika ambaye atastahili kuwa mlezi wa familia yake, na baba mzuri ambapo watoto watapata mwongozo na heshima. Mwenyezi Mungu, Mjuzi wa yote amemjaalia mwanamke uwezo usio wa kawaida. Mafanikio na furaha, na pia mateso ya familia yapo mikononi mwake.
Mwanamke anaweza kuifanya nyumba kuwa pepo ya hali ya juu au jahanamu inayowaka moto. Anaweza akamfikisha mume wake kwenye kilele cha mafanikio au balaa isiyofaa. Mwanamke mwenye sifa alizopewa na Mwenyezi Mungu, ambaye anatambua wajibu wake kama mke, anaweza kumnyanyua mume wake kuwa mtu wa kuheshimika hata kama alikuwa mtu wa chini sana kuliko wote.
Mwanachuoni mmoja aliandika: Wanawake wanao uwezo wa ajabu ambao kutokana nao wanaweza kupata chochote wanachotaka.”
Katika Uislamu, mke kumtunza mume kuna daraja la maana sana. Imelinganishwa na jukumu la Jihadi (vita takatifu katika njia ya Mwenyezi Mungu). Imam Ali (a.s) alisema: “Jihadi ya mwanamke ni kumtunza mume wake vizuri.”
Fikiria kwamba Jihadi ni mapambano na vita vitakatifu katika njia ya Mwenyezi Mungu, pamoja na mapambano ya kuendeleza heshima ya Uislamu, kulinda nchi za kiislamu na kutekeleza haki katika jamii, ni mojawapo ya matendo ya kiwango cha juu sana ya ibada.
Faida ya kutekeleza majukumu ya mke mzuri, vile vile huakisiwa wakati wa kufikiriwa kwa Jihadi.
Mtume (s.a.w.w) wa Uislamu alisema: “Mwanamke yeyote anayekufa ambapo mume wake yuko radhi naye, huingia Peponi.”
Mtume pia alisema “Kama mwanamke hatatimiza wajibu wake kama mke, hajafanya wajibu wake kwa Mwenyezi Mungu.”
Wema
Kila mtu ana hamu ya urafiki na wema. Wote wanataka kupendwa na wengine. Moyo wa mwanadamu hunemeeka kwa hilo.
Mtu ambaye hapendwi na mtu yeyote anajifikiria yeye mwenyewe kama yupo peke yake na ametelekezwa. Bibi mpendwa! Mumeo hajawa tofauti. Yeye pia anahitaji mapenzi na huba. Kabla ya kuoa mapenzi na huba ya wazazi wake yalitimiza haja hii, lakini sasa, anayo matumaini kwamba wewe ndiye utakae timiza haja hii.
Mwanaume anategemea kwa mkewe kupata urafiki na mapenzi, ambyo ni haja ya wanadamu wote. Hujitahidi sana ili apate riziki na kukufurahisha wewe.
Hushirikiana na wewe matatizo yote ya maisha, na kama mwenza wako wa kweli, anajali kukufurahisha wewe kuliko hata wazazi wako wafanyavyo. Kwa hiyo, onesha shukurani zako kwake na umpende yeye, atakupenda wewe. Mapenzi ni uhusiano wa huku na huku ambao huunganisha nyoyo.
“Mvulana wa miaka ishirini ambaye alikuja Tehran kusoma kwenye chuo Kikuu, alimpenda mjane mwenye umri wa miaka thelathini na tisa ambaye alikuwa mama mwenye nyumba wake.” Hii ni kwa sababu mwanamke huyu aliijaza nafasi tupu iliyoachwa wazi na mama yake moyoni mwake kupitia wema wake.
Kama mapenzi yanatoka sehemu zote mbili, msingi wa ndoa unakuwa na nguvu na hatari za kutengana zinaepukwa. Usifikiri kwa majivuno kwamba mumeo alikupenda wewe alipokuona mara ya kwanza, kwa sababu mapenzi ya aina hiyo hayadumu. Mapenzi yanayodumu ni yale yanayopitia kwenye wema na huba ya kudumu katika namna ya urafiki wa karibu sana.
Kama unampenda mumeo na unao urafiki mzuri naye, atafurahi na atakuwa radhi kujitahidi na kujitolea kwa ajili ya ustawi wako.
Mwanaume anayefurahia mapenzi ya mkewe, husumbuliwa na maradhi mara chache au matatizo ya mshtuko. Kama mwamaume hapewi uhusiano mwema na wa kirafiki na mkewe anaweza kukata tamaa na kuanza kuikwepa nyumba yake. Anaweza kujikuta anatumia muda wake mwingi sana katika kutafuta marafiki na watu wa kumjali. Anaweza akajisemea mwenyewe: “Kwa nini nifanye kazi na kuwasaidia watu ambao hawanitaki. Inawezekana labda nikajifurahisha mwenyewe na kujaribu kupata marafiki wa kweli.”
Mwanamke anaweza akampenda mumewe kwa uaminifu, lakini mara nyingi haoneshi au kuyadhihirishi mapenzi yake.
Haitoshi kuanzisha uhusiano wa kirafiki na kuchukulia kwamba hali hiyo ni sawa. Matamshi ya mara kwa mara kama vile, ‘ninakupenda,’ ‘umepotea machoni kwangu sana,’ Ninafurahi kukuona,’ husaidia sana kuendeleza uhusiano mzuri. Mume anapokuwa safarini, mwanamke lazima amwandikie barua kuonesha kwamba haoni raha bila kumuona.
Kama ipo simu ofisini kwa mwanamume, mke anatakiwa kumpigia simu mara kwa mara, lakini isizidi kiasi. Mke amsifu mumewe kwa marafiki na ndugu zake wakati hayupo, na kumtetea endapo mtu anamsema kwa ubaya.
Mwenyezi Mungu Mweza wa yote anazungumzia kuhusu mapatano haya ya mapenzi na huba ya mume na mke ndani ya Qur’an:
وَمِنْ آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ أَزْوَاجًا لِتَسْكُنُوا إِلَيْهَا وَجَعَلَ بَيْنَكُمْ مَوَدَّةً وَرَحْمَةً ۚ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ {21}
“Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wenza kwa ajili yenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. hakika katika haya bila shaka; zipo Ishara kwa watu wanao fikiri ”.(Quran 30:21)
Imam Ridha (a.s) alisema: “Wanawake wengine ni baraka kwa waume zao ambao huonesha mapenzi na huba yao.”
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Watu walio bora sana miongoni mwa wanawake ni wale wenye mapenzi na huba.” Imam Sadiq (a.s) alisema: “Ukimpenda mtu mwoneshe kwamba unampenda.”
Heshima Ya Mume
Hamu ya kuheshimiwa ni jambo la asili, lakini si kila mtu yupo tayari kuitoa. Mumeo hukutana na watu wengi katika shughuli zake wakati hayupo nyumbani. Baadhi ya watu hao wanaweza kuwa hawana staha na kumfedhehesha hali ambayo hatimaye humtibua mtu.
Wewe kama mke wake, anakutarajia wewe kuonesha heshima na ari akiwa nyumbani na kwa hali hiyo unaipandisha hadhi ya nafsi yake iliyokanyagwa.
Kumstahi na kumheshimu mume wako hakukudhalilishi wewe, lakini huongeza nguvu na mwelekeo kwenye harakati za kuyafanya maisha kuwa bora. Kila mara unatakiwa umsalimie na kwa hayo maamkizi yako mfanye ahisi unamjali. Usiingilie kati mazungumzo yake. Uwe na adabu na mpole unapozungumza naye na usimpigie makelele. Inapotokea wote wawili mnakwenda kwenye mkutano ngoja mumeo aingie kwanza. Msifie mbele ya watu wengine. Waambie watoto wenu kumheshimu baba yao na uwakaripie kama hawaoneshi adabu kwake. Mheshimu mbele ya wageni na uwe makini kwa mahitaji yake, na yale ya wageni.
Anapogonga mlango jaribu kufungua mlango huku ukitabasamu na kuonesha uso wenye furaha. Tendo hili dogo la kuonesha furaha, athari yake ni kwamba huburudisha moyo na kumwondolea uchovu mumeo. Baadhi ya wanawake wanaweza kudhani kwamba tabia ya aina hiyo si ya kawaida. Fikiria unapomwamkia mumeo kama mgeni. Hii si tabia nzuri kwa sababu mumeo amekuwa kwenye harakati siku nzima kwa ajili ya ustawi wa familia yake na anastahiki kufikiriwa na kuheshimiwa anaporudi nyumbani. Maamkuzi hayo ya kwanza huleta picha nzuri sana, na lililo zuri kwa mgeni ni zuri pia kwa jamaa wa familia.
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Wajibu wa mwanamke ni kujibu hodi ya mlangoni na kumkaribisha mume wake.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwanamke anayemheshimu mume wake na hamsumbui, atapata bahati na mafanikio.”
Mtukufu Mtume (s.a.w) alisema: “Mke anawajibika kutayarisha beseni na taulo ili mumewe anawe mikono.”
Uwe mwangalifu usije ukamfedhehesha mumeo, usizungumze naye kwa ukali, usimtukane, uwe msikivu kwake na usimuite kwa majina machafu. Ukimkosea na yeye atakufedhehesha wewe. Hatimaye, moyo wa mapenzi na kuaminiana utamomonyoka. Kwa hiyo, mtagombana mara kwa mara na kubishana, hali ambayo itasababisha mtalikiane.
Hata kama mtaendelea kuishi pamoja, maisha yenu kwa hakika yatajaa fujo. Hisia za uadui na usumbufu wa kisaikolojia unaweza kuanza kujengeka hadi kufikia kiwango cha kuhatarisha maisha ya wanandoa na hali hiyo inaweza kusababisha uhalifu. visa vifuatavyo vinaonesha baadhi ya mambo haya:
“Mtu mmoja mwenye umri wa miaka ishirini alimchoma kisu mkewe mwenye umri wa miaka kumi na tisa hadi akafa kwa sababu mke alimtukana mume. Mahakamani mume alisema; ‘nilimuoa mwanamke huyu mwaka moja uliopita. Mwanzoni mke wangu alinipenda sana. Lakini baada ya kipindi kifupi mke wangu alibadilika na kuanza kunidhalilisha.
Alianza kutumia lugha ya matusi kwangu kila ilipowezekana na kwa sababu ndogo sana, alianza kunikebehi. Kwa sababu jicho langu la kushoto ni kengeza, akawa na desturi ya kuniita mimi ‘punda kipofu.’ Siku moja, akaniita ‘punda kipofu’ nilikasirika sana hivyo kwamba nilimchoma kisu mara kumi na tano.’ ”
“Mtu mwenye umri wa miaka sabini na moja (71) ambaye alimuua mkewe, alitoa maelezo yafuatayo: ‘Ghafla tabia ilibadilika kwangu na akaanza kutonijali mimi. Wakati mmoja akaniita ‘mtu nisiyevumilika.’ nikagundua kwamba alikuwa hanipendi tena, nikamshuku na nilimuua kwa kumkata shoka mara mbili.”
Malalamiko Na Manung’uniko
Hakuna mtu yeyote asiyekuwa na matatizo na manung’uniko kuhusiana na maisha ya kila siku. Kila mtu hupenda kuwa na mtu wa kumhurumia ambaye anaweza kuwa mwandani wake na kumsikiliza matatizo yake. Lakini jambo la kukumbuka ni kwamba “upo wakati na mahali kwa kila jambo.” Mtu lazima aelewe wakati muafaka na mahali pa kulalamikia. Baadhi ya wanawake wajinga na wabinafsi hawatambui kwamba waume zao wanachoka sana na fadhaa baada ya kazi ya siku nzima. Badala ya kungoja kwa muda wa saa moja au mbili ili apumzike na kupata nguvu, huanza kumshambulia kwa mfululizo wa malalamiko. Mathalani mke anaweza kusema:
“uliniacha mimi na watoto hawa maluuni na ukaenda zako. Ahmad amevunja kioo cha mlango wa chumba cha mbele. Watoto wetu wa kike walipigana. Makelele ya watoto wa majirani zetu yananiudhi kweli. Hasan hajifunzi hata kidogo na amepata maksi za chini sana. Nimefanya kazi sana leo najisikia nimechoka. Hakuna hata mtu wa kusikiliza kilio changu!
“Watoto hawa hawanisaidii hata kidogo kwa kazi za hapa ndani. Afadhali nisingezaa watoto kabisa! Unayo habari dada yako alikuwa hapa leo? Sijui tatizo lake nini; alikuwa anafanya mambo kama vile nimemeza urithi wa baba yake.
“Mungu na aninusuru kutoka na mama yako! Amekuwa ananisengenya. Nimechoshwa na wote hao. Pia nimejikata kidole leo kwa kisu na kuumia sana.
“Ingekuwa vema kama nisingekwenda kwenye harusi ya Muhamedi jana. Ungemuona mke wa Rashid! Alivyopendeza, ungeshangaa! Mwenyezi Mungu angenipa na mimi bahati kama hiyo! Wanaume wengine wanawapenda wake zao na huwanunulia vitu vizuri. Hao ndio waoaji wa kweli.
“Rashid alipoingia kila mtu alimpa heshima. Ni kweli kwamba watu hupendelea kuona tu vazi ulilovaa. Anacho nini ambacho mimi sina? Kwa nini ajioneshe mbele yangu? Ndio, anayo bahati kuolewa na mume ambaye anampenda, yeye si kama wewe!
“Siwezi kuvumilia kuendelea kuishi kwenye nyumba iliyolaaniwa, kukutunza wewe na watoto. Kwa hiyo fanya utakalo!”
Msimamo wa namna hi si sahihi. Wanawake wa aina hii hudhani kwamba waume zao huondoka kwenda kwenye pikiniki au burudani kila asubuhi. Wanaume hukutana na mamia ya matatizo kila siku. Bibi mpenzi! Hujui mumeo amepita kwenye mambo gani anapokuwa katika kazi yake. Hujui ni watu fidhuli na wenye karaha kiwango gani mumeo ameshughulika nao siku nzima. Kwa hiyo, anapokuja nyumbani usiwasilishe malalamiko yako yote kwa wakati moja. Usimfanye ajihisi kuwa imekuwa hatia kuwa mwanamume.
Uwe na wastani na umfikirie. Endapo kwa kunung’unika kwako na kumsumbua, kutamuongezea wasi wasi na machungu, basi, ama anaweza akaanza ugomvi au akaondoka hapo nyumbani na kwenda kwenye mgahawa au filamu au hata kutembea tu mitaani.
Kwa hiyo, ewe Bibi mpenzi! Kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, acha mazoea haya ya kulalamika hata wakati usio muafaka. Tafuta muda unaofaa na halafu mpe matatizo yako ambayo ni ya kweli, si kwa kulalamika, lakini fanya hivyo, kwa namna ya kushauriana. Kwa njia hii, hutasababisha yeye kuanza kujenga hisia za uadui na mapatano ya familia yanabaki kuwa salama.
Mtume (s.a.w.w) wa Uislamu alisema:
“Sala za mwanamke anayemchokoza mume wake kwa ulimi wake, hazikubaliwi na Mwenyezi Mungu hata kama akifunga saumu kila siku, anaamka kila siku usiku kufanya ibada, anawaachia huru watumwa katika njia ya Mwenyezi Mungu. Mwanamke mwenye ulimi mbaya ambaye humuumiza mumewe kwa njia hii, ni mtu wa kwanza kuingia Jahanamu!”
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) pia alisema: “Wanawake wa Peponi huwaambia wanawake wanaowatukana waume zao kwa njia hii: ‘Mwenyezi Mungu na akuuweni. Msiwe watovu wa adabu kwa waume zenu. Mtu huyu (mume) si kiumbe wako, na wewe hustahiki kuwa naye. Muda mfupi ujao atakuacha na atakuja kwetu.’ ”
Sijui wanawake wa aina hii wanataka kujipatia nini kwa hayo manung’uniko yao. Kama wanataka kusikilizwa na waume zao au kujionesha, basi, hakika wanajipatia kitu kinyume chake kabisa na kumkasirisha. Kama wanakusudia mateso kwa mume, kumsababishia madhara ya kisaikolojia na kumuingiza kwenye mazoea bandia ya kuangamiza, basi wapo kwenye njia potofu.
Bibi mpendwa! Kama unamjali mumeo na familia yako, basi ni lazima uache msimamo huu usio na mantiki. Je, umewahi hata kufikiria kwamba mwenendo wako mbaya unaweza ukasababisha kuvunjika kwa maisha ya familia yako?
“Daktari mmoja alitoa ushahidi mahakamani: ‘Sijapata kumuona mke wangu akifanya mambo kama mke sahihi wa nyumbani wakati wote wa ndoa yetu. Nyumba yetu mara nyingi imekuwa katika machafuko.Wakati wote mke wangu anapiga makelele na kutukana. Nimechoshwa naye.’ Baada ya kumlipa mke wake fedha nyingi tu, akapata talaka. Akasema kwa furaha: ‘Kama angetaka na angeomba utajiri wangu wote na hata shahada yangu ya taaluma ya tiba, ningempa ili niachane naye haraka sana.’ ”
Tabia Za Kupendeza
Mtu yeyote mwenye tabia njema na inayopendeza pia angepata dhiki na matatizo ya maisha kwa njia ile ile. Hawa ni aina ya watu ambao watu huvutiwa nao na wanawatafuta wakati wote. Tabia inayopendeza na msimamo wa mtu utakuwa na kinga dhidi ya maradhi ya kisaikolojia kwa kuwa kuonekana kwao katika maisha ni kushinda matatizo yao kwa njia nzuri iwezekanayo.
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Hakuna maisha yanayo kubalika zaidi kuliko yale ambayo yanatokana na tabia njema.”
Lakini mtu mwenye tabia mbaya naye pia angeyaona maisha hayafurahishi kwani uhusiano wa watu hao kuendeleza wasiwasi na fadhaa.
Mtu kama huyu hupenda kulalamika na kupigia kelele maisha. Msimamo wa namna hii huepukwa na watu wengi ambapo mtu huyo hapati marafiki wengi. Hii ndio hali ambayo huathirika kwa urahisi na matatizo mbali mbali ya kisaikolojia na maradhi mengineyo kwa sababu ya wasi wasi na utupu ambao mtu mwenye msimamo mbaya anavyoyaona maisha.
Mtukufu Mtume (s.a.s) alisema: “Mtu mwenye tabia na msimamo mbaya atakuwa kwenye masumbuko na mateso wakati wote.”
Msimamo mzuri na unaopendeza ni muhimu kwa watu wote kwa ujumla na hususan baina ya wanandoa kwani wanandoa lazima wawe pamoja.
Mpendwa Bibi! Kama unataka kufurahia maisha ya furaha na mumeo na watoto wako, ufanye msimamo wako na tabia ya kupendeza vikubalike. Uwe na tabia njema na si mgomvi. Unao uwezo wa kuifanya nyumba yako kuwa Pepo ya hali ya juu au Jahanamu iwakayo moto. Unaweza kuwa malaika wa huruma ambapo mumeo na watoto wanaweza kupata amani kupitia kwako.
Unajua utaacha mvuto wa kupendeza kiasi kwenye roho zao kwa huo msimamo wako wa kutabasamu na lugha nzuri.
Mvuto wa kupendeza ni mbichi katika akili zao wanapoondoka kwenda shuleni au kwenye shughuli za kazi na unawasaidia wao kuwa na mwanzo mzuri wa siku.
Kwa hiyo, kama unajali kuhusu sifa nzuri ya maisha yako na uhusiano ulio nao na mumeo, usiwe kinyume na tabia njema. Uwe dhahiri katika msimamo wako na tabia inayopendeza kwani nguzo bora zaidi ya kutegemea kwa usalama wa ndoa ni maadili mazuri ambayo yanaelekeza kwenye tabia inayopendeza.
Namna nyingi za talaka ni kwa sababu ya tabia zisizolingana za mume na mke. Takwimu juu ya talaka kwa uthibitisho zinaonesha kwamba msimamo wa kupatana, maadili mema na tabia ya kupendeza, hazikuwepo kwa wanandoa husika. Chanzo kikubwa cha ugomvi na kutokuelewana kwa wanandoa ni kwa sababu yakutolingana kwa tabia na kanuni za maadili za wanandoa. Takwimu zifuatazo zinavutia:
“Mwaka 1968 kesi za malalamiko ya ndoa zilizowasilishwa mahakamani zilikuwa 16,039, kesi 12,760 miongoni mwa hizo, misingi ya malalamiko yao ilikuwa kutokulingana kwa kanuni za maadili. Mwaka 1969 kesi za malalamiko ya aina hiyo hiyo 16,058 liziwasilishwa mahakamani, kesi 11,246 miongoni mwa kesi hizo, misingi ya malalamiko ilifanana na ile ya kesi za mwaka wa nyuma. Kwa hiyo, inathibitika kwamba zaidi ya asilimia sabini ya ugomvi wa kifamilia ulisababishwa na kipengele hiki.”
Mwanamke alilalamika kwenye Baraza kwamba mume wake kila siku alikuwa na desturi ya kula chakula chake cha mchana na jioni nje.
Halafu mwanaume akaeleza kwamba sababu iliyomfanya ale nje ni kwamba mke wake hakuwa mbunifu hata kidogo na alikuwa mwenye tabia isiyopendeza kuliko wanawake wote wenye tabia kama hiyo hapa duniani. Haraka sana mwanamke alinyanyuka na kuanza kumpiga mume wake mbele ya majaji.”
Mwanamke huyu mpumbavu alidhani kwamba angebadilisha tabia ya mume wake ya kula chakula chake nje badala ya nyumbani kwa kulalamika, kutukana na kumpiga.
Lakini mwanamke huyu hakutumia mbinu rahisi na ya kiakili ambapo alitakiwa kuwa na busara zaidi na kuzingatia mwenendo unaostahili.
Mwanamke mwingine alipeleka taarifa mahakamani kwamba mume wake aliacha kusema naye kwa muda wa miezi 15 na kwamba alikuwa anatoa matumizi yake kupitia kwa mama yake (mume). Mume alijibu kwamba alikwisha kinai na msimamo usiopendeza wa mke wake ambao ulimfanya yeye asizungumze naye kwa miezi.”15
Migongano mingi ya kifamilia inaweza kusuluhishwa kwa wema, huruma na tabia inayopendeza. Kama mume wako si mwema, kama anatoka kwenda kula chakula cha jioni peke yake, kama anapenda kutumia lugha ya matusi, anatumia utajiri wake wote vibaya, hupenda kusema suala la kutalikiana na kutengana au sababu kadhaa katika ugomvi wa kifamilia, ipo njia moja tu ya kusuluhisha. Njia hii ni kuwa mwema na tabia njema. Matokeo ya mazoea ya tabia kama hii ni ya kimiujiza.
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwenyezi Mungu Mweza wa yote atampa mtu mwenye tabia ya kupendeza thawabu zinazolingana na zile za Jihadi. Atamneemesha kwa wingi mtu huyo usiku na mchana.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwanamke yeyote anaye msumbua na kumtesa mumewe yu mbali na neema za Mwenyezi Mungu na mwanamke yeyote anayemheshimu, anaye mtii na hamhuzunishi mumewe, ameneemeka na kufanikiwa.”
Ipo hadith inayosema kwamba Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alipewa taarifa ya mwanamke mwema ambaye alifunga saumu kila siku na alikuwa anafanya ibada kila siku usiku akimuabudu Mwenyezi Mungu, lakini alikuwa na tabia isiyo pendeza ya kuwaudhi majirani zake kwa maneno yake makali. Mtukufu Mtume alisema: “Hapana jema kwake huyo na yeye ni mkazi wa Jahanamu.”
Matarajio Mabaya
Mpendwa Bibi! Wewe ni mwanamke mkuu wa familia yako. Uwe na hekima na uweledi. Panga vizuri matumizi yako. Panga bajeti ya matumizi yako kwa njia ambayo haitasababisha hasara kwa utajiri na hekima yako.
Usishindane na wengine na uwaonee wivu. Kama unaona nguo nzuri imevaliwa na mwanamke, au kama unavutiwa na fanicha na vyombo ambavyo umeviona kwenye nyumba ya rafiki, usimlazimishe mumeo kununua vitu kama hivyo ambavyo vinazidi uwezo wake wa kifedha na pengine atalazimika kukopa. Je, si vema zaidi kungoja hadi hapo ambapo hali ya kipato itaruhusu au itakapopatikana akiba ya ziada ya kuwezesha kununua vitu visivyo vya muhimu?
Mara nyingi ni wale wanawake wajinga na wanaojipendelea ambao hushindwa, na kuwa wabadhirifu na kutaka kushindana. Wanawake wa aina hii huwalazimisha waume zao kuingia kwenye madeni na huchoshwa na kukasirishwa na kujaribu kuridhisha matakwa yao yasiyo weza kutoshelezwa. Wakati mwingine, ufumbuzi wa aina moja tu uliopo kwa wanaume wa kutatua matatizo haya ni uamuzi wa kumtaliki mke au kujiua.
Wanawake ambao hawatambui madhumuni ya kweli na maana ya ndoa na badala yake wanaifikiria kama utumwa ambapo mwanamume anapatikana kwa lengo la kutimiza matamanio yao ya kitoto na mahitaji ya kiulimwengu.
Wanawake wa namna hii wanataka mume ambaye atawahudumia kama mtumwa na hawatapinga njia zao za matumizi. Wanawake wa aina hii mara nyingine huenda mbali zaidi. Wanawafanya waume zao watumie zaidi ya uwezo wao hali ambayo inaweza kuwafilisi, wanaweza kufanya mauaji au matokeo yoyote ya msiba.
Wanawake wa aina hii ni aibu kwa wanawake wenzao. Endapo matarajio yake makubwa yanasababishwa kutalikiana, mwanamke atanyang’anywa mapenzi ya watoto wake na ataishi maisha ya upweke.
Kwa wanawake wa aina hii si rahisi kuolewa tena kwa urahisi. Hata kama inatokea, hakuna uhakika wa ndoa ya pili kama itadumu, kwani binadamu wengi hawapendi kuwekwa katika utumwa. Na mume mpya inawezekana naye asiwe na uwezo wa kutimiza mahitaji yao kabisa kuliko hata wa mwanzo.
Mpendwa Bibi! Badala ya kuwa mwenye tamaa sana, jaribu kuwa mwenye busara. Tumia muda mwingi na juhudi kwa ajili ya ustawi wa familia yako na mumeo badala ya kujaribu kuiga mambo ya kila mtu. Kama mumeo anaumia kupita kiasi, mzuie na udhibiti matumizi yake yasiyo ya muhimu. Badala ya kununua bidhaa zisizo za muhimu, ni vema kuweka kiasi fulani cha akiba kwa ajili ya matatizo ya siku za usoni.
Katika hadith Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke yeyote ambaye halingani na mume wake na humshawishi afanye mambo zaidi ya uwezo wake, basi matendo yake hayatakubaliwa na Mwenyezi Mungu, ataonja ghadhabu ya Mwenyezi Mungu mnamo Siku ya Ufufuo.”
Katika hadith nyingine, Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke yeyote asiyelingana na mumewe, haridhiki na kile ambacho Mwenyezi Mungu amewajaalia na humtendea mume wake ubaya kwa kudai ampe zaidi ya uwezo wake, basi matendo yake (au ibada ya mke) hayakubaliki kwa Mwenyezi Mungu na Atamkasirikia mwanamke huyo.”
Katika hadith nyingine, Mtume (s.a.w.w) alisema: “Baada ya kumwamini Mwenyezi Mungu, hapana neema iliyo kubwa zaidi ya kuwa na mume au mke mnayeelewana naye.”
Uwe Faraja Kwa Mumeo
Uzito wa mzigo wa maisha huchukuliwa na wanaume kwa sababu wao wanao wajibu wa kutunza na kusaidia familia zao. Katika kutimiza wajibu huu, mwamaume wa familia lazima akabiliane na matatizo mengi na vikwazo vingi nje ya familia yake. Baadhi ya matatizo haya yanaweza kuwa ukubwa wa kazi, mizozo kwenye msongamano wa magari na usumbufu wa kungoja na kupanda mabasi kutoka nyumbani kwenda ofisini na kurudi nyumbani, wasiwasi kuhusiana na masuala ya marafiki nawafanyakazi wenzake na wasiwasi wa kiuchumi na kisiasa ya siku hiyo, wasi wasi wa marafiki na wafanya kazi wenzake, na wasiwasi wa kujaribu kuboresha hali ya maisha ya familia yake. Kiasi cha mishughuliko na wasiwasi wa mtu mwenye kuwajibika ni mikubwa na yenye sehemu nyingi. Si jambo la kushangaza kwamba wastani wa umri wa mwanaume ni mdogo zaidi ya ule wa mwanamke.
Ili mwanadamu aweze kwenda sambamba na mizigo ya maisha ni muhimu kuwa na mtu ambaye atakusikiliza na kukuhurumia. Mumeo ni mmoja wapo wa watu hao. Anaweza akahisi yu mpweke na akahitaji kupata kimbilio na faraja akiwa katikati ya misukumo hii. Ni kawaida kwamba mwanaume hutarajia kupata faraja na utulivu kutoka kwa mke wake na familia yake. Kwa hiyo, tazamia matarajio na mahitaji yake.
Uwe mkunjufu na mchangamfu wakati ambapo kwanza ndio anarudi nyumbani kutoka katika kazi zake, na apate viburudisho au umfanye ahisi kwamba wewe upo tayari kusikiliza mahitaji yake. Jaribu kutokumwingiza kwenye shari kwa kuanza kumlaumu mara tu umuonapo.
Ngoja apumzike na apate nguvu upya kabla ya kumweleza madai binafsi ya watu wa familia.
Mumeo anapokuja nyumbani, jaribu kutabasamu na kumsalimia kwa uchangamfu. Mtimizie mahitaji yake ya kimwili ya uchovu, njaa na kiu. Halafu muulize kuhusu matatizo yake. Kama hayupo tayari kusema uwe msikilizaji mzuri na umhurumie. Jaribu kuonesha kuhusika kwako kwa dhati na halafu umsaidie kutambua kwamba matatizo si kwamba hayawezekani, na makubwa kama anavyodhani. Mpe moyo wa kumuunga mkono na kumsaidia aweze kukabiliana na masuala ipasavyo. Unaweza kusema kitu kama: “Matatizo haya yanawapata watu wengi. Kwa utashi na uvumilivu, inawezekana kuyatatua matatizo almuradi mtu asiruhusu yamshinde. Matatizo haya, kwa kweli ni mitihani na pia hujenga tabia ya kweli ya mtu. Usikate tamaa. Unaweza kuyatatua kwa kuazimia na ustahamilivu.
Kama unayo mawazo fulani kuhusu jinsi ya kuyashughulikia, mwaambie mumeo. Kama huna, labda unaweza kumshauri amuone rafiki mzuri ambaye anao ujuzi na sifa zaidi.
Mpendwa Bibi! Wakati wa matatizo, mumeo anahitaji sana umjali na mapenzi yako. Unatakiwa umsaidie na umtunze kama mtaalamu wa maradhi ya akili na mke mwenye huruma. Kiwango gani cha matunzo mtaalamu wa maradhi ya akili angempa ambacho na wewe ungempa? Usikadirie pungufu uwezo wako wa kumtuliza na kumpa nguvu. Hakuna mtu muaminifu na mwenye kuhusika zaidi kuhusu ustawi wa mumeo isipokuwa wewe. Ataweza kupata nguvu kutokana na mapenzi yako kwake na aweze kukabiliana na matatizo yake kwa hali ambayo itapunguza mhemuko wake na wasiwasi wa akili. Hatimaye, mapatano ya kuheshimiana na upendo utakuwa mkubwa zaidi.
Katika hadith, Imam Sadiq (a.s) alisema: “Hakuna kitu bora zaidi duniani kuliko kuwa na mke mwema. Na mke mwema ndiye huyo ambaye mume wake hufurahi pindi amuonapo.”
Kwenye hadith, Imam Rida (a,s) alisema: “Lipo kundi la wanawake ambalo huzaa watoto wengi. Ni wanawake wema na wana huruma. Huwasaidia waume zao wakati wa matatizo na katika mambo ya dunia hii na ile ijayo. Wanawake hawa hawafanyi matendo yoyote ambayo yangewapa hasara waume zao kuongeza matatizo yao.”
Uwe Mtu Wa Kuonesha Shukrani
Kama mtu ni mwema na mpaji wa utajiri wake ambao ameupata kutokana na kazi ngumu, shukrani na kuoenasha kufurahia kwako kwa matendo kama hayo ni hali ambayo itachangamsha hisia zake za ndani na kumfanya ahisi amefanikiwa.
Matendo ya ukarimu yanaweza kuwa kawaida ya mtu ambapo hujenga mazoea kutumia na kugawana utajiri wake na wale wanao hitaji. Hata hivyo, kama matendo ya ukarimu yanapuuzwa na hayafurahikiwi, mhusika anaweza akapoteza utashi na msukumo wa kufanya wema. Itakuwa ni kawaida kwa mtu kuhitimisha kwamba ilikuwa ni kutumia vibaya kutoa fedha yake aliyoipata kwa jasho ambapo hakuna shukrani inayotolewa.
Shukrani na kufurahishwa ni tabia za kuvutia akiwa nazo mtu na ni siri ambayo kwayo mtu anaweza kuvuta matendo ya msaada.
Hata Mwenyezi Mungu ametaja kwamba shukrani kwa neema Zake ni sharti ambalo husababisha neema Zake kuendelea kutolewa kwa wanadamu:
وَإِذْ تَأَذَّنَ رَبُّكُمْ لَئِنْ شَكَرْتُمْ لَأَزِيدَنَّكُمْ ۖ وَلَئِنْ كَفَرْتُمْ إِنَّ عَذَابِي لَشَدِيدٌ {7}
“Na alipotangaza Mola wenu : Mkishukuru nitakuzidishieni; na mkikufuru, basi adhabu yangu ni kali.” (Qur’ani 14:7).
Mpendwa Bibi! Mumeo naye pia ni binadamu. Kama mtu mwingine yeyote yule. Yupo tayari kusaidia familia yake na anaiona kama wajibu wa uadilifu na kisheria. Anapopewa shukrani na kufurahikiwa kwa kutekeleza kazi yake, kazi hizo haziwi tena mzigo kwake.
Wakati wowote anaponunua vitu vya nyumbani au kitu kama nguo na viatu kwa ajili yako na watoto, furahi na umshukuru yeye. Onesha shukrani zako kwa vitu vidogo anavyofanya kama kununua bidhaa za vyakula, kusafiri na familia na kukupa wewe fedha. Unapoonesha shukrani, unamfanya mumeo ajihisi kuwa mwema na kuzawadiwa kwa usumbufu uliompata. Uwe mwangalifu kwamba usizipuuze kazi zake na kuwa mtu asiyejali mchango wake kuhusu ustawi wa familia.
Anaweza akaanza kutumia fedha yake kwingineko au kwake yeye mwenyewe.
Ikiwa tu rafiki au ndugu amekupa zawadi ya jozi ya soksi au shada la maua, unatakiwa kumshukuru mara nyingi, hivyo, ni kawaida tu na ni haki kumfurahia mumeo kwa kukupendelea na kukufikiria. Usidhani kwamba utakuwa unajidhalilisha kwa kuonesha shukrani zako. Kinyume chake, utapendwa na kujaliwa kwa vitu vingi zaidi kwa sababu unafurahia juhudi ya mumeo ambapo dharau na ubinafsi ni tabia ambazo zinaweza kuipeleka familia kwenye mabalaa.
Zifuatazo ni Hadith zinazozungumzia tabia za shukrani: Imam Sadiq (a.s) alisema: “Wanawake bora zaidi miongoni mwa wanawake wenu ni hao ambao huonesha furaha wakati waume zao huleta kitu nyumbani na hawaoneshi kutokuridhika kama hakuna kilicho letwa nyumbani.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwanamke yeyote ambaye husema kwa mumewe kwamba hajaona vitu vyovyote vizuri kutoka kwake basi anakuwa amekosa uaminifu na anavuruga ibada yake.”
Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alisema: “Yeyote asiye washukuru watu wanaomsaidia, kwa kweli, haoneshi shukrani zake kwa Mwenyezi Mungu kwa neema Zake.”
Usitafute Dosari Za Mwenzio
Hakuna mtu aliyekamilika. Watu wengine ni warefu sana au wafupi sana au wanene sana au wembamba sana, wanapua kubwa au pua ndogo, wanasema sana au wakimya sana, wana hasira zana au wanaelewana na watu haraka sana weusi sana rangi ya wastani au wanakula sana au wanakula kidogo na orodha inaweza kuendelea. Wanaume na wanawake wengi sana wanazo dosari hizi. Ni matumaini ya kila mwanaume na kila mwanamke kutafuta mwenzi aliyekamilika, lakini matumaini ya aina hiyo si sahihi. Hakuna uwezekano wa kumpata mwanamke anaye muona mumewe kama mtu aliye kamilika.
Wanawake hao ambao hutafuta makosa ya waume zao bila shaka watayapata.
Wanaweza wakaona dosari ndogo na kuzikuza kwa kushughulikia jambo hilo hadi kiwango cha kuwa kipingamizi kisichovumilika. Dosari hii huchukua nafasi ya sifa zingine zote za mume. Kila mara huwalinganisha waume zao na wanaume wengine. Wameanzisha kitu kinachoitwa mwanaume anayefaa katika dhana yao kiwango ambacho hakiafikiani na waume zao. Kwa hiyo, kila mara wanalalamika kuhusu dosari ndani ya ndoa zao. Wanawake hao hujifikiria kuwa na bahati mbaya na kushindwa na maisha na pole pole huwageuza kuwa wanawake |wenye chuki.
Tabia ya aina hiyo ya mwanamke humfanya nini mumewe? Anaweza kuwa ni mtu mvumilivu sana ambaye anaweza kustahamili ujeuri lakini upo uwezekano mkubwa atafedheheshwa na atakuwa na kinyongo kwa mkewe.
Hali hii inawezekana ikawatumbukiza wanandoa husika kwenye mabishano na kuelezana dosari za kila mwanandoa. Wote wawili watadharauliana na maisha yao yatageuka kuwa na mlolongo wa ugomvi na mabishano. Hivyo, ama wataishi katika mateso wakiwa pamoja au wataamua kutalikiana. Katika hoja zote mbili, wote watahasarika, hususan ambapo hakuna uhakikisho kwamba ndoa nyingine inaweza kuthibitisha vinginevyo.
Inasikitisha kwamba wapo wanawake wasiojua na wanakaidi katika huo ujinga wao. Inawezekana kwamba wanaweza kuharibu maisha ya familia zao kwa jambo dogo. Ifuatayo ni mifano ya wanawake wa aina hiyo: “Mwanamke alimwacha mume wake na akaenda nyumbani kwa baba yake kwa sababu mume wake alikuwa ananuka mdomo. Mwanamke huyo hakuwa tayari kurudi kwa mumewe hadi atatue tatizo lake. Kufuatana na malalamiko ya mume, mahakama iliwasuluhisha wana ndoa hao na mke akarudi kwa mumewe. Walipokwenda nyumbani, mke aligundua kwamba pumzi ya mumewe ilikua bado inanuka, kwa hiyo alihamia chumba kingine.”
“Daktari wa meno mwanamke alimtaliki mume wake kwa sababu hakuwa katika kiwango kinacholingana na cha kwake; mwanaume alifuzu na kupata taaluma hiyo miaka mitatu baada ya mke wake.”
“Mwanamke aliomba kumtaliki mume wake kwa sababu alikuwa na desturi ya kuketi chini na kula kwa kutumia vodole vyake, alikuwa hanyoi kila siku na hakujua jinsi ya kuishi na watu.”
Kama mambo yalivyo, si kwamba wanawake wote wapo hivi. Wapo wanawake wenye akili, wa kweli, na wanao utambuzi wa kutosha kwamba hawa hatarishi ndoa na furaha kwa kukuza dosari za waume zao. Mpendwa Bibi! Mumeo ni binadamu kama wewe. Hakukamilika, lakini anaweza kuwa na sifa nyingi. Kama unapendezwa na ndoa yenu na familia yenu basi usitafute udhaifu wake.
Usifikirie dosari zake ndogo kuwa muhimu. Usimlinganishe na mwanaume huyo ambaye umembuni akilini mwako. Inawezekana mumeo awe na udhaifu fulani ambao haupo kwa wengine. Lakini kumbuka kwamba wanaume wengine wanaweza kuwa na kasoro ambazo hazipo kwa mumeo. Ridhika na sifa zake. Hatimaye, utaona kwamba sifa zake zinazidi dosari zake. Zaidi ya hayo kwa nini utarajie kumpata mume mkamilifu ambapo wewe mwenyewe si mkamilifu. Kama wewe unajivuna kiasi cha kutosha kujiona wewe ni mkamilifu, basi waulize watu wengine:
Mtume (s.a.w.w) alisema: “Hakuna kitu kibaya zaidi kwa binadamu kuliko kutafuta dosari za watu wengine, ambapo hawajali mapungufu yao.”
Kwa nini ukuze dosari ndogo? Kwa nini uharibu maisha yako kwa kitu kisichokuwa maanani?
Uwe na busara, acha upuuzi! Puuza dosari za mumeo na usizitaje mbele yake au nyuma yake. Jaribu kutengeneza hali ya hewa ya uchangamshi katika familia yako na ufurahie neema za Mwenyezi Mungu.
Hata hivyo, inawezekana pawepo dosari katika tabia ya mumeo ambazo unaweza kuzirekebisha. Kama ni hivyo, unaweza kufaulu kufanya hivyo hapo tu ambapo utakuwa na busara na uvumilivu. Hutakiwi umlaumu au kuanza kumgombeza, lakini mwendee kwa njia ya kirafiki.
Usimwangalie Mtu Yeyote Isipokuwa Mumeo
Mpendwa Bibi! Kabla hujaolewa inaewezekana ulikwisha chumbiwa na watu wengine. Posa za uchumba huu inawezekana zilitoka kwa watu matajiri, wasomi, wenye sura nzuri na kadhalika ambao ungependa wakuoe.
Matarajio ya aina hiyo yalikuwa ni jambo la kawaida kabla ya kuolewa. Lakini sasa umechagua mwenzi wako na kuwekeana mkataba wa dhati naye kuwa wapenzi katika maisha yenu yote, hivyo, sahau yaliyopita kabisa. Lazima uyaweke pembeni matamanio yako ya zamani na usahau ofa hizo za zamani. Usimfikirie mwamanume mwingine yeyote isipokuwa mumeo na utafute amani naye. Kama ukifanya vinginevyo, utajiweka katika hali ya mashaka.
Sasa basi, umekubali kuishi na mumeo, kwa nini wakati wote uendelee kuwatilia maanani wanaume wengine? Kwa nini umlinganishe mumeo na wanaume wengine? Unapata manufaa gani unapowatazama na kuwatilia maanani wanaume wengine isipokuwa kujiweka katika hali ya mateso yasiyo na mwisho na kusababisha upate maumivu makali ya akili?
Imam Ali (a.s) alisema: “Yeyote anayeyaacha macho yake huru, kila mara atapata maumivu ya neva na atanasa kwenye mtego wa wivu wakati wote.”
Kwa kuwatazama waume wengine na kuwatilia maanani na kuwalinganisha na mumeo, utamuona mwanaume ambaye hana dosari za mumeo. Unaweza kudhani kwamba labda mwamaume huyo amekamilika kwa sababu huzijui dosari za mwanaume huyo. Utafikiria kuwa ndoa yako ina mushkeli, na fikira hii inaweza ikawafikisheni mahali penye mwisho wenye hatari.
Mke wa mtu, umri wake miaka 18 ambaye alitoroka nyumbani kwake alikamatwa na polisi usiku wa jana. Akiwa kituo cha polisi mwanamke huyu alisema kwamba baada ya miaka mitatu ya ndoa, pole pole alihisi kwamba hampendi mume wake. Alisema: “Nilikuwa na tabia ya kulinganisha uso wa mume wangu na nyuso za wanaume wengine na nikajuta kwa nini niliolewa naye.”
Mpendwa Bibi! kama unataka ndoa ya kudumu daima milele, kama hutaki mateso ya kiakili, na kama unataka muendeshe maisha ya kawaida, basi acha kuwa mbinafsi na sahau hayo matarajio yako yasiyofaa. Usiwapongeze wanaume wengine. Usimfikirie mwanaume yeyote isipokuwa mumeo. Usiendekeze fikira hizi:
‘Afadhali ningeolewa na fulani’
‘Ningependa mume wangu aonekane kama . . . . . .’
‘Natamaani mume wangu angefanya kazi ya. . .. . . . . .’
‘Natamaani….. Natamaani……. Natamaani….’
Kwa nini ujifunge jela kwa kuendekeza mawazo hayo? Kwa nini utibue misingi ya ndoa yako? Kama lolote kati ya matakwa hayo yangefanikiwa kwa kweli, ungejuaje kwamba ungefanikiwa kuridhika zaidi? Unao uhakika kwamba wake za waume wajulikanao kama ‘hawana dosari; wanaridhishwa nao?
Mpendwa Bibi! Kama mumeo anashuku kwamba unaonesha kuvutiwa na wanamume wengine, atakata tamaa na kuacha kuvutiwa na wewe. Usitaniane na wanamume wengine au kufuatana nao. Wanamume ni wepesi kuhisi hivyo kwamba hawawezi hata kuvumilia wake zao kuonesha kuvutiwa na picha ya mwanamume mwingine.
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke yeyote aliyeolewa ambaye huwatazama wanamume wengine atakabiliwa na adhabu kali ya Mwenyezi Mungu.”
Vazi La Hijabu La Kiislamu
Wanaume na wanawake, licha ya kwamba wanavyo vipengele vingi vinavyofanana, pia wanazo tabia za pekee. Mojawapo ya tabia hizi ni kwamba wanawake ni viumbe wa kuvutia, wazuri, na wanaopendwa. Ni wachangamfu, wanavutia na wanapendwa; ambapo wanaume huchangamshwa, huvutiwa na huwapenda wanawake kwa sifa zao.
Mwanaume anapomuoa mwanamke, hutamani uzuri wote na mapenzi yote ya mke wake visitiriwe kwa ajili yake tu.
Hutumaini kuwa ni yeye peke yake ndiye anayefaidi uchangamfu, mapenzi, kujishaua, uzuri, ukunjufu na kadhalika na kuwaepuka wanaume wengine kabisa. Mwanaume kimaumbile yu moto moto sana na hamvumilii mwanaume mwingine kumtazama mke wake au kuanzisha aina fulani ya uhusiano naye. Mwanaume ataona uhusiano wa karibu na mke wake na wanaume wengine kuwa ni kukiukwa kwa haki yake ya kisheria. Mume anatarajia mkewe kufuata kanuni ya vazi la kiislamu la Hijab na kwa kuwa mwepesi wa kubadilika kufuatana na tabia na maadili ya Kiislamu atashiriki katika kutunza haki yake ya kisheria.
Mwanaume yeyote aliye mwaminifu na hamasa lazima atakuwa na hamu hiyo. Tabia ya kijamii ya mwanamke ambayo imeegemezwa kwenye maadili ya Kiislamu, itaweka akili ya mume katika hali ya utulivu; kwa hiyo atafanya kazi kwa shauku kubwa ili aweze kutunza familia yake, na mapenzi kwa mke wake yataongezeka. Mwanaume wa namna hii hatavutiwa na wanawake wengine. Kinyume chake mwanaume ambaye mkewe havai Hijab ambayo ni vazi linalovaliwa na mwanamke Mwislamu na badala yake huonesha uzuri wake kwa wanaume wengine au anachanganyika nao, atatibuliwa sana. Atamuona mke wake kuwa anahusika na kukandamiza haki zake. Mume wa aina hiyo kila mara atapitia kwenye mateso na taabu na mapenzi kwa mkewe yatapungua pole pole.
Kwa hiyo, ni kwa manufaa ya jamii, na wanawake kwamba wanatakiwa kuvaa inavyostahiki na kuwa na tabia ya unyenyekevu, wanatakiwa kuonekana hadharani bila urembo na kuacha kuonesha uzuri wao kwa wengine.
Kuvaa Hijab ni wajibu wa Kiislamu. Mwenyezi Mungu Mweza wa yote anasema kwenye Qur’ani Tukufu:
وَقُلْ لِلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا ۖ وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ ۖ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُولِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَىٰ عَوْرَاتِ النِّسَاءِ ۖ وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِنْ زِينَتِهِنَّ ۚ وَتُوبُوا إِلَى اللَّهِ جَمِيعًا أَيُّهَ الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ {31}
“Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho Yao, Na wazilinde tupu zao, na wala wasioneshe uzuri wao isipokuwa unaodhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasioneshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au watoto wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyowamiki mikono yao ya kuume, au wafuasi wanamume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yanayohusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajulikana mapambo waoliyoyafisha. Na tubuni vyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa. (Quran 24:31)
Kuchunga vazi la Kiislamu la Hijab na kuizingatiwa matumizi yake katika jamii kuna manufaa kwa wanawake katika vipengele vingi: Kwa kutumia vazi la Hijab, wanawake wanaweza kulinda uzuri wao wa kijamii na maadili ya ndani kwa ubora zaidi, na kujilinda dhidi ya kuwa tu kitu kilichopo kwenye maonesho.
Wanaweza kuthibitisha imani na mapenzi yao kwa waume zao, kwa ukamilifu zaidi na kwa hiyo kusaidia kutengeneza na kutunza familia yenye uchangamfu na kuzuia hisia mbaya na ugomvi wa kifamilia. Kwa ufupi, wanaweza kuvutia nyoyo za waume zao na kujiimarisha kwenye familia zao.
Kwa kuzingatia matumizi ya Hijab ya Kiislamu mitazamo isiyo ya kisheria yenye dokezo ya kutamani kutoka kwa watu wenye udhaifu huo, itakoma na kusaidia kupunguza idadi ya ugomvi, kuimarisha mizizi ya familia, na matokeo yake kutengeneza mazingira ya utulivu ndani ya familia.
Hijab ya Kiislamu ya wanawake pia itasaidia vijana wa kiume ambao hawajaoa, kutokana na kujiingiza kwenye vitendo viovu. Hivyo, kuwaepusha vijana dhidi ya mazingira yanayoamsha hisia za kutamaani mwanamke aliyevaa nguo isiyo sitiri umbo lake hali ambayo pia itawanufaisha wanawake katika jamii.
Kama wanawake wote wangefuata utaratibu wa Hijab ya Kiislamu basi, wanawake wote wangekuwa na uhakika kwamba waume zao wanapokuwa nje ya familia zao, hawangekutana na mwanamke asherati ambaye angewavutia na kumtoa nje ya familia yake.
Uislamu unatambua lengo mahususi ambalo limesababisha kuumbwa kwa mwanamke na humuona yeye kama msingi muhimu wa jamii na kupewa wajibu kwa jamii. Jamii humtaka mwanamke ajitolee katika kutekeleza wajibu wake wa kuvaa Hijab ya Kiislamu, ambayo ingeepusha uovu na upotofu wa jamii na kutengeneza uimara, usalama na kutukuza taifa lake. Lakini kwa wazi wazi thawabu kubwa zaidi ni kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mweza wa yote kwa kutekeleza wajibu wake kwa dini.
Mpendwa Bibi! Kama unapenda uimara na amani kuwepo kwenye familia yako, na mumeo aendelee kukuamini wewe siku zote, kama unajihusisha na haki za wanawake katika jamii; kama unavutiwa na afya ya vijana kiakili na unao wasi wasi kwamba wanaweza wakaacha maadili mema, kama unataka kuchukua hatua za uhakika za wanaume waovu kuacha kuwatongoza wanawake; na kama unatafuta radhi ya Mwenyezi Mungu kwa kuwa Muislamu muaminifu na mwenye kujitolea, basi tumia vazi la Hijabu ya Kiislamu.
Usioneshe uzuri wako na urembo wako kwa wageni, ama uwe ndani nyumbani kwako ukiwa na ndugu zako wa karibu, au kwenye mikusanyiko mingine ya kijamii nje ya nyumbani kwako. Lazima uvae ushungi mbele ya shemeji zako na watoto wao, waume wa wifi zako, waume wa shangazi zako, na binamu zako.
Usipovaa Hijabu ya Kiislamu mbele ya watu waliotajwa ni dhambi na pia unaweza kusababisha mateso makubwa kwa mumeo, hata kama hatasema.
Mwanamke halazimiki kuvaa Hijabu kwa kiwango kile kile mbele ya baba mkwe, kaka yake, na watoto wa kiume wa kaka au dada yake, ingawa ni vema kwa kiwango fulani kuvaa Hijabu mbele ya watu hawa pia. Kwa usemi mwingine, wanawake wasionekane mbele ya watu hawa- ndugu zake- kama ambavyo anaweza kuvaa kwa kumvutia mumewe. Hii ni kwa sababu wanaume wengi sana hawapendi wake zao waonekane katika hali ya kuvutia kwa kuvaa nguo au urembo mbele ya wanaume wengine, na kama mambo yalivyo isisahaulike kwamba utulivu wa akili na imani ya mume kwa mke wake ni muhimu sana kwa kudumu na usalama wa familia yote.
Samehe Makosa Ya Mumeo
Kila mtu isipokuwa wale ambao Mwenyezi Mungu amewatangaza kuwa
‘Maasum’
hufanya makosa. Watu wawili wanaopendana na wanashirikiana pamoja, hufanya makosa, lazima wawe wasemehevu. Kama hawatasameheana, basi ndoa yao itavunjika.
Wafanya biashara wawili ambao ni wabia, na jirani wawili, marafiki wawili na hususan mume na mke wanahitaji kusameheana.
Kama watu wa familia hawasameheani na kufuatilia makosa ya kila mmoja wao, basi ama familia itafarakana au wataishi maisha yasiyovumilika.
Mpendwa Bibi! Pengine mumeo hufanya makosa. Anaweza akakutukana, akakufedhehesha, akasema uwongo, anaweza hata kukupiga. Matendo kama hayo yanaweza kufanywa na mwanamume yeyote.
Baada ya kufanya kosa, kama mumeo hujuta kwa kosa hilo au wewe unahisi anajuta kwa kosa lake hilo, basi msamehe na usilifuatilie jambo hilo. Kama anajuta lakini hayupo tayari kuomba msamaha, basi usijaribu kuthibitisha kosa lake. Vinginevyo, anaweza kuhisi anadhalilishwa na anaweza kulipiza kisasi kwa kukumbuka makosa yako na kwa hiyo, ikawa chanzo cha ugomvi mkubwa kwa hali hiyo, ni bora wewe unyamaze kimya hadi hapo atakapo jilaani mwenyewe kutoka kwenye dhamira yake na akaanza kuhisi majuto kuhusu kosa hilo. Hapo atakuona wewe kuwa ni mtu mwenye busara na mke wa kujitoa kwa mambo mema ambaye anavutiwa na mume wake, na familia yake.
Mtume (s.a.w.w) wa Mwenyezi Mungu alisema: Mwanamke mbaya hatoi msamaha kwa makosa ya mumewe na hakubali hata kuomba msamaha.”
Je, si ni jambo la kusikitisha kwamba mkataba wa ndoa takatifu unavunjwa kwa sababu mwanamke hayupo tayari kusamehe makosa fulani ya muewe?
Kuweza Kuishi Na Ndugu Wa Mumeo
Mojawapo ya matatizo ya kifamilia husababishwa na ndugu wa mume na mke wake.
Baadhi ya wanawake hawana uhusiano mzuri na mama wa mumewe, dada au kaka zake mumewe.
Kwa upande moja mke anaweza kujaribu kumtawala mume wake ili asiweze kumsikiliza hata mama yake au ndugu yake yeyote na anaweza kujaribu kuwafitinisha ili wasielewane wao kwa wao. Kwa upande mwingine, mama wa mume anajiona kuwa yeye ni mmiliki wa mwanae na mke wa mwanae.
Mama hujaribu sana kuwa karibu sana na mwanae na kutahadhari kwamba mke wa mwanae asiweze kummiliki mumewe kwa ukamilifu. Anaweza kusingizia uwongo kuhusu mke wa mwanae au kumuona anayo makosa.
Msimamo wa aina hii unaweza kufuatwa na mabishano mengi na hata chuki ya mara kwa mara. Hali inakuwa mbaya zaidi endapo watu hawa huishi kwenye nyumba moja. Hata kama ugomvi unaweza kutokea baina ya wanawake wawili, uchungu wa kiakili na dhiki hasa zaidi humpata mume aliyoko kati yao.
Mume ananaswa katikati ya mabishano ambapo hawezi kuegemea upande wowote. Kwa upande moja yupo mke wake ambaye angependa kuendesha maisha ya kujitegemea bila kuingiliwa na mtu yeyote. Kwa kawaida mume huhisi lazima amsaidie mke wake na amfurahishe. Lakini kwa upande mwingine, anafikiria wazazi wake ambao wamemsaidia kuingia katika maisha, wamemsomesha na wametumia muda mwingi wa maisha yao kumlea.
Anahisi kwamba wazazi wake wanatarajia awasaidie wakati wanahitaji msaada na kwamba haitakuwa busara kuwasahau. Zaidi ya hayo, kama yeye mwenyewe anayo haja ya kupata kitu fulani, hatakwenda kwingineko isipokuwa kwa wazazi wake, ambao watamsaidia yeye na familia yake. Matokeo yake ni kwamba anatambua kwamba marafiki zake wakuaminika ni wazazi wake na ndugu zake. Kwa hiyo, mtanziko kwa mtu mwenye busara ni ama kuwa upande wa mke na kuwaacha wazazi au kinyume chake, lakini hapana lolote kati ya haya mambo mawili yanawezekana.
Matokeo yake, atalazimika kwenda na pande zote mbili na kuziweza pande hizi katika hali ya kuridhika ambayo ni kazi ngumu. Njia moja tu inayoweza kurahisisha hali ni kwamba mwanamke lazima awe mwaminifu na mwenye hekima. Katika hali kama hii, mume anatarajia mkewe amsaidie katika kutatua tatizo.
Kama mke anamheshimu mama mkwe wake, humtaka ampe ushauri wake, na anakuwa mtiifu na kufanya urafiki naye basi, mama mkwe wake atakuwa msaidizi wake mkubwa sana.
Je, si jambo la kusikitisha kuona mtu ambaye anaweza kuwavutia watu wengi kwa sababu ya wema wake na tabia zake, halafu awafukuze kwa ajili ya ukaidi na ubinafsi wake? Hutambui kwamba katika mazuri na mabaya ya maisha, mtu anaweza akahitaji msada wa wengine, na hususan ule wa ndugu ambao wanaweza kukusaidia ambapo kila mtu akiwa amekukimbia? Je, si ni jambo zuri zaidi kufurahia uhusiano mzuri na ndugu wa mtu kwa kutumia busara na tabia njema? Je, hivi kweli ni busara na haki kufanya urafiki na watu wengine ambapo unavunja uhusiano na ndugu zako?
Uzoefu unaonesha kwamba mtu anapotaka msaada kutoka kwa wengine, marafiki humkimbia lakini ndugu aliwo watupa huja kumsaidia. Hii ni kwa sababu mshikamano wa kifamilia unao asili na hauwezi kuvunjika kwa urahisi. Kuna methali isemayo: “Hata kama nyama ya mtu ingeliwa na ndugu zake, wasingeitupa mifupa yake”
Imam Ali (a.s) alisema: “Mtu hawezi kamwe kuishi bila kuwa na ndugu zake, hata kama ni tayari na anao watoto.”
Mtu atataka heshima na wema wa ndugu zake. Ni wao ndio watakao msaidia kimwili na kiakili. Ni ndugu ndio wanasaidia mara nyingi. Wakati wa shida ndugu huweza kusaidia haraka zaidi kuliko wengine. Yeyote anaye watupa ndugu zake hupoteza mikono mingi, ya kumsaidia.
Mpendwa Bibi! Kwa ajili ya mume wako na faraja yako mwenyewe na pia kutafuta marafiki wengi na wanao kuunga mkono, vumilia kuwa nao ndugu wa mumeo. Usiwe mbinafsi na mjinga; uwe na busara na usisababishe usumbufu wowote kwa mumeo. Uwe mke mzuri na mwenye kujitolea ili uweze kukubalika kwa Mwenyezi Mungu na watu.

Comments
Post a Comment