Ni vipi vinywaji vinavyolewesha? Je, nini mtazamo wa Uislamu kuhusu vinywaji vinavyolewesha?

Dear Brother / Sister,
Vinywaji vinavyolewesha ni vinywaji vinavyoondosha uwezo wa kufikiri sawa sawa na kujenga hoja na kusababisha hali ya ulevi (kutokujitambua).
Kur’an inakataza vinywaji vinavyolewesha na kutaja kabisa kwamba ni haramu: “Enyi mlio amini! Bila ya shaka ulevi, na kamari, na kuabudu masanamu, na kupiga ramli, ni uchafu na ni kazi ya Shet'ani. Basi jiepusheni navyo, ili mpate kufanikiwa.” (al-Maida, 5/90). Wanazuoni wengi wanasema kwamba kinachomaanishwa kwenye neno “hamr” (Vilevi) kwenye aya inahusisha vinywaji vyote vinavyoondoa akili. Wafuasi wa madh-hebi ya Hanafi wanaelezea hamr kama ifuatavyo:  Vinywaji ambavyo vimetengenezwa kwa zabibu tu na kuwa na povu jingi huitwa hamr. Vinywaji vyengine vinavyolewesha watu havizingatiwi kama hamr. Vinazingatiwa kama hamr kupitia hoja za kimantikivikilinganishwa na madhara ya ulevi.. Wanazuoni wengi wa fiqh wanasema kwamba vinywaji vyote ambavyo huwafanya watu kulewa ni haramu ima ikiwa ni kwa kiwango kidogo au kikubwa kwa ujumla  huitwa hamr. . (Tafsiri ya Sahih Muslim, na maelezo, A. Davudoğlu, IX, 247, ff.)
Sambamba na Uislamu, kunywa kilevi ni haramu vile vile kwenye dini zote za mbinguni zilizopita. Sentensi zifuatazo kwenye Agano la Kale, kwenye kitabu kitukufu cha Wayahudi, ni maarufu sana:
“Kisha BWANA akanena na Haruni, na kumuambia, Usinywe divai wala kileo chochote, wewe, wala wanao pamoja nawe, hapo mwingiapo ndani ya hema ya kukutania, ili kwamba msife; amri hii itakuwa amri ya milele katika vizazi vyenu; kisha mpate kupambanua kati ya yaliyo matakatifu na hayo yaliyo ya siku zote, na kati ya yaliyo najisi na hayo yaliyo safi;” (Agano la Kale, Mambo ya Walawi, 10, mstari wa 8, 9-11)
Yafuatayo yametajwa kwenye Agano Jipya: “Nao walipokuwa wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndio damu yangu ya agano, imwagikapo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu” (Agano Jipya, Matayo 26,26-29, Yohana 30: n.k)
Inajulikana kwamba Waturuki walikuwa Washamani kabla ya Uislamu. Inajulukana kwamba walikuwa wanakunywa vinywaji tofauti kama kumis hasa wakati wa sherehe na sherehe za kuweka wakfu kwa dini hiyo. (Mehmet Aydın-Osman Cilacı, Dinler Tarihi, Konya 1980, uk. 97 ff.)
Kabla ya Uislamu na kipindi cha mwanzo wa Uislamu, Waarabu wajinga, walikuwa wanakunywa ulevi na kuona kama sehemu ya maisha yao ya kila siku. Uislamu ulitoa umuhimu mkubwa kwenye kulinda mambo makubwa matano: Akili, afya, mali, heshima na dini. Mtu anaekunywa pombe hawezi kuvilinda vitu hivi vitano. Taasisi moja iliyoanzishwa kwa mara ya kwanza nchini Marekani kutafiti ni nani aliyekataza unywaji wa pombe duniani. Walipogundua kwamba katazo la kwanza liliteletwa na Hz. Muhammad, walijenga mnara wa kumbukumbu pale New York iloitwa “Chemchem ya Muhammad” ndani ya New York kwa ajili ya kumkumbuka. (Yeşilay Dergisi, iss. 441, August 1970)
Makatazo ya ulevi yalitolewa kwenye Kur’an kwa hatua taratibu.
Kwenye aya ya kwanza inayozungumzia ulevi ambayo ilishushwa Makka, hakukutajwa katazo lolote.
“Na kutokana na matunda ya mitende na mizabibu mnatengeneza vinyaji vinavyofaa na riziki nzuri. Tazama katika hayo ipo Ishara kwa wanao tumia akili.” (an-Nahl, 16/67)
Baada ya hayo, Hz. Umar alikwenda kwa Mjumbe wa Allah (rehma na Amani ziwe juu yake) mara moja na akamuambia, “Ewe Mjumbe wa Allah! Hivi unajua kama divai huharibu mali na huondoa akili. Muombe Allah ashushe hukumu kuelezea divai. Kisha Hz. Mtume akaomba ifuatavyo: “Ewe Allah! Tushushie hukmu yako kuhusu divai.” Baada ya hapo ikashuka aya ifuatayo:
“Wanakuuliza juu ya divai na kamari. Sema: Katika hivyo zipo dhambi kubwa na manufaa kwa watu. Lakini dhambi zake ni kubwa zaidi kuliko manufaa yake.” (al-Baqara, 2/219). Wakati aya hii inashushwa , baadhi ya Maswahaba waliacha pombe wakasema, “ni dhambi kubwa” lakini wengine waliendelea kunywa wakisema, “ina manufaa kwa mwanadamu”.
Mara moja, Abdurrahman b. Awf alifanya sherehe na baadhi ya Maswahaba walikuwa katika sherehe hii. Baadhi yao wakanywa pombe. Ulipofika muda wa swala ya maghrib (jioni), mmoja wao aliongoza swala na akasoma aya katika suratul “al-Kafirun” kimakosa. Baada ya hapo, Hz. Umar akaomba kama ifuatavyo: “Ewe Allah! Ongeza sheria kuhusu ulevi!!” Baadae, aya ifuatayo ikashushwa: “Enyi mlio amini! Msikaribie Sala, hali mmelewa, mpaka myajue mnayo yasema.” (an-Nisa, 4/43). Kwa hivyo, kunywa pombe ikakatazwa muda wa swala tu. Wale waliokuwa wanakunywa pombe walianza kunywa baada ya swala ya usiku (isha) na kuswali swala ya asbuhi baada ya ulevi kuisha/kuisha.
Mara moja Utba b. Malik (radhi za Allah ziwe juu yake) alifanya sherehe ya harusi. Sa`d b. Abi Waqqas alikuwepo pia. Walikula ngamia, wakanywa pombe na wakaanza kujigamba kwa utukufu wao. Sa`d akasoma shairi la kusifu kabila lake na kuwafanyia mzaha Ansar. Mmoja katika Ansar akakasirika na akamjeruhi Sa`d kwa mfupa wa ngamia. Sa`d akamlalamikia Mtume wa Allah (rehma na Amani ziwe juu yake) kuhusu Ansar. Baada ya hapo, aya zilizoelezea makatazo ya pombe kwa ujumla zikashuka:
“Enyi mlio amini! Bila ya shaka ulevi na kamari, na kuabudu masanamu, na kupiga ramli, ni uchafu na ni kazi ya Shet'ani. Basi jiepusheni navyo, ili mpate kufanikiwa. Hakika Shet'ani anataka kutia kati yenu uadui na chuki kwa ulevi na kamari, na akuzuieni kumkumbuka Mwenyezi Mungu na kusali. Basi je, mmeacha?” (al-Maida, 5/90-91)
Hadithi mbalimbali za Hz. Mtume zinaonesha umuhimu wa kutekeleza agizo hili:
“Kila kileweshacho ni ulevi na kila ulevi ni haramu. Ikiwa mtu atakunywa ulevi duniani akafa bila kutubu, hawezi kunywa maji katika mto Kauthar kesho akhera.” (Muslim, Ashriba, 73)
“Ikiwa kitu kinalewesha ima kwa kiwango kikubwa au kidogo pia ni haramu.” (al-Asqalani, Bulughu`l Maram, Imetafsiriwa na A. Davudoğlu, lV, 61, ff)
Wakati Hz. Mtume alipoulizwa kuhusu amri ya ulevi, alisema, “Bila shaka yoyote, ulevi si dawa; na kinyume chake, ni matatizo.” (al-Asqalani, ibid, IV, 61)
“Baadhi ya watu katika Umma wangu watakunywa vilevi wakivipa majina tofauti tofauti.” (al-Asqalani, ibid, IV, 61)
Kuna maafikiano/makubaliano ya umma kwamba ulevi umekatazwa.
Wanazuoni wa Kiislamu wanakubaliana juu ya jambo hili bila shaka/kwa kauli moja. Ingawa, kuna kutokukubaliana kwenye baadhi ya vinywaji hasa kwa baadhi ya mujtahid. Ili kuondosha shaka hizo, Hz. Umar aliweka maana fupi yenye kueleweka kwenye neno la Mjumbe wa Allah kwenye mimbari: “Kila kinachoondoa akili ni ulevi.”  Kwahiyo, kila kitu kinachopoteza akili ya mwanadamu na kumfanya asiweze kutofautisha lipi zuri na lipi baya na lipi lina manufaa na lipi lina madhara huzingatiwa kama ulevi. Haijalishi kama ni kimiminika au yabisi (kitu kigumu).
Opiamu, heroini na madawa ya kulevya yanayofanana na hayo yanazingatiwa ni sawa na kilevi kwasababu kazi za akili hubadilika kwa watumiaji; huanza kuviona vitu vya mbali kuwa vipo karibu na vitu vilivyo karibu kama vipo mbali; huanza kuvikimbia vitu vya kawaida na kuanza kufikiria vitu vinavyowezekana na visivyowezekana, wakiishi kwenye ulimwengu wa ndoto. Baadhi ya madawa huufanya mwili kukosa nguvu, kudhoofisha mfumo wa hisia (neva), kusababisha msongo wa mawazo, kudhoofisha nguvu za utashi na kumfanya mtu si lolote si chochote kwenye jamii. Dini ya Kiislamu inaagiza mambo ya manufaa kwa mtu mmoja mmoja na kwa jamii na kukataza yenye madhara. Wakati makatazo ya Uislamu yakichunguzwa kitabibu, yanagundulika kwamba yapo kwa ajili ya manufaa ya jamii. Ukweli ni kwamba, makatazo kama ulevi na nyama ya nguruwe yalichunguzwa na wanasayansi na matabibu, na madhara ya kivitu na kiroho yakaelezwa na wataalamu. (angalia Yusuf al-Qardawi, al-Halal wa`l-Haram fi`l-Islam, Imetafsiriwa na Mustafa Varlı, Ankara 1970, p. 50-53, 75-88).
Uislamu unakataza kunywa pombe na biashara yake baina ya Waislamu vilevile. Hz. Mtume amewalaani watu kumi kutokana na ulevi: mtu anaetengeneza, anaetengenezewa, anaekunywa pombe, anaebeba, anaebebewa, anaesababisha watu kunywa (mhudumu), anaeuza, anaetumia pesa itokanayo na ulevi, anaenunua, na anaenunuliwa…” (Tirmidhi, Buyu`, 59; Ibn Majah, Ashriba, 6).
Baada ya aya katika Suratu al-Maidah ambayo imeelezea katazo la kunywa pombe, Mjumbe wa Allah alieleza yafuatayo kuhusu kutekeleza: “Kwa hakika Allah amekataza vinywaji vinavyolewesha. Mtu anaesikia aya hii na ana vinywaji vya ulevi hatakiwi kunywa au kuviuza…” (Muslim, Musakat, 67; angalia Bukhari, Maghazi, 51; Buyu, 105, 112; Muslim, Buyu, 93; Far', 8; Ibn Majah, Tijarat, 11; Ahmad b. Hanbal, II, 213, 362, 512, III, 217, 324, 326, 340; Ibn Kathir, Mukhtasar Tafsir Ibn Kathir, Beirut (n.d), I, 544-547).

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KUSWALI HATUA KWA HATUA

Maana ya kufunga Maana ya kufunga katika Uislamu: Ni kufanya ibada kwa ajili ya Allah kwa kujizuia na kuacha kula, kunywa, kujamiiana, pamoja na vitu vyote vyenye kufunguza, kuanzia kuchomoza kwa alfajiri –ambao ni muda wa adhana ya Alfajiri- mpaka kuzama kwa jua – ambao ni muda wa adhana ya Magharibi-. «...Basi atakayekuwa katika mji (hayuko safarini) miongoni mwenu katika mwezi (wa Ramadhani) aufunge». Sura Albaqara, aya 185. Ubora wa mwezi wa Ramadhani Mwezi wa Ramadhan ni mwezi wa tisa katika miezi ya mwezi muandamo katika kalenda ya Kiislamu. Ni mwezi bora zaidi katika mwaka. Allah ameuhusisha peke yake kuliko miezi mingine kwa sifa nyingi bora na za kipekee, na miongoni sifa hizo bora ni hizi: Kwamba Ramadhan ni mwezi ambao Allah ameuhusisha na kushuka kwa Qur’ani kitabu kitukufu na bora kuliko vitabu vyote. Allah Mtukufu amesema kuwa: «Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa humo Qur’ani ikiwa ni muongozo kwa watu, na hoja zilizo wazi za muongozo na upambanuzi. Basi atakayekuwa mjini miongoni mwenu katika mwezi huu, basi afunge». (Sura Albaqara, aya 185) Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Utakapoingia mwezi wa Ramadhani milango ya pepo hufunguliwa, na milango ya Jahanamu hufungwa, na mashetani hufungwa minyororo». (Bukhari, Hadithi Na. 3103, Muslim, Hadithi Na. 1079). Hakika Allah ameuandaa mwezi huu kwa waja wake ili waelekee kwake kwa kufanya ibada na kuacha maovu. Kwamba mwenye kufunga mchana wa Ramadhani na akasimama usiku wake (kwa kuswali), Allah humsamehe madhambi yake yaliyopita. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga Ramadhani kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, Hadithi Na. 1910, Muslim, Hadithi Na. 760). Pia Mtume amesema kuwa: «Mwenye kusimama (kwa kuswali) katika Ramadhani kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, hadithi na. 1905, Muslim, Hadithi Na. 759). Kwamba ndani ya mwezi wa Ramadhani kuna usiku wenye hadhi kubwa (Lailatul Qadri), usiku ambao ni bora sana kuliko nyakati nyingine za usiku za mwaka mzima. Allah ameeleza katika kitabu chake kwamba kufanya jambo jema ndani ya usiku huo ni bora zaidi kiliko kulifanya jema hilo siku nyingi nyingine. Allah amesema kuwa: «Lailatulqadri ni bora zaidi kuliko miezi elfu moja». (Sura Alqadri, aya 3). Mwenye kusimama katika usiku huo kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah husamehewa madhambi yake. Huo ni usiku uliopo katika siku kumi za mwisho katika mwezi wa Ramadhani, na hakuna yeyote anayejua tarehe yake kwa uhakika. Ubora wa kufunga «Ambaye hakuacha kusema uzushi na kuutumia hakuna haja kwa Allah katika kuacha chakula chake na kinywaji chake». Kufunga kuna fadhila nyingi ambazo zimeelezwa katika sheria. Miongoni mwazo ni hizi zifuatazo: Kwamba mwenye kufunga mwezi wa Ramadhani kwa kumuamini Allah, kutii amri zake, kuamini fadhila zake zilizotajwa na sheria na kuwa na matarajio ya kupata thawabu kwa Allah, atasamehewa madhambi yake yaliyopita. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga Ramadhan kwa kuamini kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, Hadithi Na. 1910, Muslim, Hadithi Na. 760). Pia mwenye kufunga atafurahia malipo atakayoyapata wakati wa kukutana na Mola wake kwa sababu ya funga yake. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga ana furaha mbili: furaha wakati wa kufungua kwake na furaha wakati wa kukutana na Mola wake». (Bukhari, Hadithi Na. 1805, Muslim, Hadithi Na.1151) Peponi kuna mlango unaoitwa Arrayaan. Haingii yeyote kupitia mlango huo isipokuwa tu wenye kufunga. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Hakika, peponi kuna mlango unaoitwa Arrayyaan. Wenye kufunga wataingia kupitia mlango huo Siku ya Kiama. Haingii yeyote kupitia mlango huo ila wao tu. Patatolewa tangazo kwamba: Wako wapi wenye kufunga? Watasimama. Hataingia yeyote kupitia mlango huo isipokuwa wao tu. Wakishaingia, utafungwa na hataingia yeyote kupitia hapo». (Bukhari, hadithi Na. 1797, Muslim, Hadithi na. 1152) Pia Allah ameyahusisha kwake yeye tu malipo na thawabu za mfungaji. Ikiwa malipo ya mtu yanatoka kwa Mkarimu, Mtukufu, Mtoaji sana na Rahimu sana, anatakiwa ayafurahie yale ambayo Allah amemuandalia. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, katika Hadithi Qudsiy amesema kuwa: «Matendo yote ya mwanadamu ni yake yeye isipokuwa funga. Funga ni yangu, na mimi ndiye nitakaye itolea malipo». (Bukhari, Hadithi Na. 1805, Muslim, Hadithi Na.1151) Hekima ya funga Allah amefaradhisha kufunga Ramadhani kwa hekima nyingi na faida mbali mbali katika dini na dunia, na miongonimwazo ni hizi: Kuthibitisha kumtii Allah na kumuogopa. Hiyo kutokana na kuwa funga ni ibada ambayo mja anajiweka karibu ya Allah kupitia ibada hiyo kwa kuacha anavyo vipenda, na kuyazuia mataminio yake. Anaidhibti nafsi yake kwa kumcha Allah na kumuogopa kila sehemu na kila wakati, katika siri na katika dhahiri. Kwa sababu hii, Allah Mtukufu anasema kuwa: «Enyi mlio amini, mmefaradhishiwa kufunga kama walivyofaradhishiwa waliokuwepo kabla yenu ili mpate kuwa wenye kumuogopa Allah». (Sura Albaqara, aya 183) Mazoezi ya kuacha maasi na madhambi Mwenye kufunga ajizuiapo kufanya mambo yaliyo halali kwa kufuata amri ya Allah atakuwa na uwezo zaidi wa kuyadhibiti mataminio yake ya kutaka kufanya maasi na madhambi, atachunga mipaka ya Allah na hatajiachia katika kufanya maovu. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mtu ambaye haachi kusema uzushi na kuufanyia kazi, basi Allah hana haja ya kuacha chakula chake na kinywaji chake». (Bukhari, Hadithi Na. 1804). Maana ni kwamba: Mtu ambaye haachi uongo na kufanya uchafu katika kauli na vitendo, huyo hajayafikia makusudio ya funga. Kuwakumbuka wenye shida na kuwasaidia Hiyo inatokana na kwamba katika funga kuna mazoezi ya kupambana na ukata, njaa, na kuwakumbuka maskini ambao wanapambana na hali ya kutokuwa na pato la kutosha siku zote. Kwa kufunga, mja huwakumbuka ndugu zake masikini na namna wanavyoteseka na mambo mawili machungu; njaa na kiu, na kwa sababu hiyo, atafanya juhudi ya kuwasaidia na kuwafariji.

UTUKUFU WA MJI WA MAKKA NA MSIKITI MTUKUFU