NAFASI YA FAMILIA KATIKA UISLAMU

Namna Uislamu unavyoijali familia unaonekana wazi katika mambo yafuatayo:
  1. Uislamu umetilia mkazo sana suala la kuoa na kuanzisha familia. Umelifanya suala hilo kuwa ibada kubwa sana na ni katika mwenendo wa Mitume. Amesema Mtume, swallalahu alayhi wasalam, kuwa: «Lakini mimi ninafunga swaumu na ninafungua. Ninaswali usiku na ninalala,  na ninaoa wanawake. Kwa hiyo, mwenye kupinga mwenendo wangu (huu) sio mwenzangu». (Bukhariy, Hadithi Na. 4776. Muslim, Hadithi na. 1401)
  • Qur`ani inahesabu kwamba yale mambo ambayo Allah ameyaumba kwa mume na mkewe, ikiwa ni pamoja na utulivu, mapenzi, huruma na kuliwazika ni miongoni mwa neema, alama na miujiza mikubwa sana. Amesema Allah Mtukufu kuwa: «Na ni miongoni mwa alama zake kwamba amekuumbieni wake watokanao na nyinyi ili mpumzike kwao, na akajaalia baina yenu mapenzi na huruma».(Arruum, aya 21)
  • Uislamu umeamrisha suala la ndoa lifanywe jepesi na kumsaidia anayetaka kuoa ili apate hifadhi. Amesema Mtume, swallalahu alayhi wasalam, kuwa: «Watu wa aina tatu ni haki kwa Allah  kuwasaidia watu hao» na akataja miongoni mwa watu watatu hao kuwa ni, «..na muoaji ambaye anakusudia kujihifadhi». (Tirmidhiy, Hadithi Na. 1655).
  • Uislamu umewaamrisha vijana ambao wako katika kilele cha ujana wao na nguvu zao kwamba waoe, kwa sababu katika kuoa kuna utulivu na suluhisho la kisheria la  kukidhi nguvu za matamanio yao. 
Uislamu unaichukulia ndoa na kujenga familia kuwa ni miongoni mwenendo wa Mitume, na umeamrisha kulifanya jambo hilo kuwa jepesi na kuwasaidia vijana walifanye.
  1. Uislamu umempa heshima kamili kila mtu katika familia, sawa awe mwanamke au mwanaume:
Uislamu umembebesha baba na mama majukumu makubwa ya kulea watoto wao. Imenukuliwa kwa Abdallah Bin Omar, Allah amuwiye radhi, akisema kuwa  alimsikia Mtume wa Allah akisema kwamba: «Kila mmoja wenu ni mchungaji, na ataulizwa juu ya kile alichokichunga.  Imamu ni mchungaji na ataulizwa juu ya kile alichokichunga. Na mwanaume ni mchungaji katika familia yake, naye ataulizwa juu ya kile alichokichunga. Na mwanamke ni mchungaji katika nyumba ya mume wake, naye ataulizwa juu ya kile alichokichunga. Na mtumishi ni mchungaji katika mali ya mwajiri  wake, naye ataulizwa juu ya kile alichokichunga».(Bukhariy, Hadithi Na. 853. Muslim, Hadithi Na. 1829)
  1. Uislamu umefaradhisha kwa Muislamu kuimarisha udugu. Maana ya kuimarisha udugu ni Muislamu kuwa na mawasiliano mazuri na ndugu zake wa upande wa baba na mama na kuwafanyia mambo ambayo ni mazuri: 
Kama vile kaka na wadogo zake, dada zake, ami zake na watoto wao, shangazi zake, wajomba zake, mama zake wakubwa na wadogo na watoto wao. Uislamu umelihesabu jambo hilo kuwa ni miongoni mwa ibada kubwa sana. Pia Uislamu umekataza kuwakatia udugu au kuwafanyia mambo mabaya, na umelihesabu jambo hilo kuwa ni miongoni mwa madhambi makubwa sana. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Haingii peponi mtu mwenye kukata udugu».(Bukhariy, Hadithi Na. 5638. Muslim, Hadithi Na. 2556)
  1. Uislamu umehimiza kupanda mbegu ya msingi wa kuwa na adabu na heshima kwa wazazi, kuwahudumia na kuwatii mpaka kufa:
Mtoto wa kike au wa kiume hata kama ni mtu mkubwa kiasi gani, ni wajibu kwao kuwatii wazazi wao na kuwafanyia mambo mazuri. Allah amelikutanisha pamoja jambo hilo na kuabudiwa kwake. Pia amekataza kuwakosea adabu kwa vitendo au maneno, hata kama hilo litafanyika kwa kutamka wazi neno moja au sauti inayo onesha kukerwa nao. Allah Mtukufu amesema kuwa: «Na Mola wako amehukumu kwamba msiabudu (chochote) isipokuwa yeye tu na kuwanfanyia wazazi mambo mazuri. Kama mmoja wao atafikia uzee au wote wawili ukiwa nao, basi usiwaambie hata Ah!  wala usiwafokee, na sema nao kwa maneno mazuri».(Al-israa,aya 23)
  1. Kufanya uadilifu kwa watoto
Uislamu umeamrisha kulinda haki za watoto wakike na wakiume katika matunzo na mambo ya dhahiri. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mcheni Allah na fanyeni uadilifu kwa watoto wenu». (Bukhariy 2650).

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KUSWALI HATUA KWA HATUA

Maana ya kufunga Maana ya kufunga katika Uislamu: Ni kufanya ibada kwa ajili ya Allah kwa kujizuia na kuacha kula, kunywa, kujamiiana, pamoja na vitu vyote vyenye kufunguza, kuanzia kuchomoza kwa alfajiri –ambao ni muda wa adhana ya Alfajiri- mpaka kuzama kwa jua – ambao ni muda wa adhana ya Magharibi-. «...Basi atakayekuwa katika mji (hayuko safarini) miongoni mwenu katika mwezi (wa Ramadhani) aufunge». Sura Albaqara, aya 185. Ubora wa mwezi wa Ramadhani Mwezi wa Ramadhan ni mwezi wa tisa katika miezi ya mwezi muandamo katika kalenda ya Kiislamu. Ni mwezi bora zaidi katika mwaka. Allah ameuhusisha peke yake kuliko miezi mingine kwa sifa nyingi bora na za kipekee, na miongoni sifa hizo bora ni hizi: Kwamba Ramadhan ni mwezi ambao Allah ameuhusisha na kushuka kwa Qur’ani kitabu kitukufu na bora kuliko vitabu vyote. Allah Mtukufu amesema kuwa: «Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa humo Qur’ani ikiwa ni muongozo kwa watu, na hoja zilizo wazi za muongozo na upambanuzi. Basi atakayekuwa mjini miongoni mwenu katika mwezi huu, basi afunge». (Sura Albaqara, aya 185) Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Utakapoingia mwezi wa Ramadhani milango ya pepo hufunguliwa, na milango ya Jahanamu hufungwa, na mashetani hufungwa minyororo». (Bukhari, Hadithi Na. 3103, Muslim, Hadithi Na. 1079). Hakika Allah ameuandaa mwezi huu kwa waja wake ili waelekee kwake kwa kufanya ibada na kuacha maovu. Kwamba mwenye kufunga mchana wa Ramadhani na akasimama usiku wake (kwa kuswali), Allah humsamehe madhambi yake yaliyopita. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga Ramadhani kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, Hadithi Na. 1910, Muslim, Hadithi Na. 760). Pia Mtume amesema kuwa: «Mwenye kusimama (kwa kuswali) katika Ramadhani kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, hadithi na. 1905, Muslim, Hadithi Na. 759). Kwamba ndani ya mwezi wa Ramadhani kuna usiku wenye hadhi kubwa (Lailatul Qadri), usiku ambao ni bora sana kuliko nyakati nyingine za usiku za mwaka mzima. Allah ameeleza katika kitabu chake kwamba kufanya jambo jema ndani ya usiku huo ni bora zaidi kiliko kulifanya jema hilo siku nyingi nyingine. Allah amesema kuwa: «Lailatulqadri ni bora zaidi kuliko miezi elfu moja». (Sura Alqadri, aya 3). Mwenye kusimama katika usiku huo kwa kuamini na kutaraji kupata malipo ya Allah husamehewa madhambi yake. Huo ni usiku uliopo katika siku kumi za mwisho katika mwezi wa Ramadhani, na hakuna yeyote anayejua tarehe yake kwa uhakika. Ubora wa kufunga «Ambaye hakuacha kusema uzushi na kuutumia hakuna haja kwa Allah katika kuacha chakula chake na kinywaji chake». Kufunga kuna fadhila nyingi ambazo zimeelezwa katika sheria. Miongoni mwazo ni hizi zifuatazo: Kwamba mwenye kufunga mwezi wa Ramadhani kwa kumuamini Allah, kutii amri zake, kuamini fadhila zake zilizotajwa na sheria na kuwa na matarajio ya kupata thawabu kwa Allah, atasamehewa madhambi yake yaliyopita. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga Ramadhan kwa kuamini kutaraji kupata malipo ya Allah, husamehewa madhambi yake yaliyopita». (Bukhari, Hadithi Na. 1910, Muslim, Hadithi Na. 760). Pia mwenye kufunga atafurahia malipo atakayoyapata wakati wa kukutana na Mola wake kwa sababu ya funga yake. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mwenye kufunga ana furaha mbili: furaha wakati wa kufungua kwake na furaha wakati wa kukutana na Mola wake». (Bukhari, Hadithi Na. 1805, Muslim, Hadithi Na.1151) Peponi kuna mlango unaoitwa Arrayaan. Haingii yeyote kupitia mlango huo isipokuwa tu wenye kufunga. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Hakika, peponi kuna mlango unaoitwa Arrayyaan. Wenye kufunga wataingia kupitia mlango huo Siku ya Kiama. Haingii yeyote kupitia mlango huo ila wao tu. Patatolewa tangazo kwamba: Wako wapi wenye kufunga? Watasimama. Hataingia yeyote kupitia mlango huo isipokuwa wao tu. Wakishaingia, utafungwa na hataingia yeyote kupitia hapo». (Bukhari, hadithi Na. 1797, Muslim, Hadithi na. 1152) Pia Allah ameyahusisha kwake yeye tu malipo na thawabu za mfungaji. Ikiwa malipo ya mtu yanatoka kwa Mkarimu, Mtukufu, Mtoaji sana na Rahimu sana, anatakiwa ayafurahie yale ambayo Allah amemuandalia. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, katika Hadithi Qudsiy amesema kuwa: «Matendo yote ya mwanadamu ni yake yeye isipokuwa funga. Funga ni yangu, na mimi ndiye nitakaye itolea malipo». (Bukhari, Hadithi Na. 1805, Muslim, Hadithi Na.1151) Hekima ya funga Allah amefaradhisha kufunga Ramadhani kwa hekima nyingi na faida mbali mbali katika dini na dunia, na miongonimwazo ni hizi: Kuthibitisha kumtii Allah na kumuogopa. Hiyo kutokana na kuwa funga ni ibada ambayo mja anajiweka karibu ya Allah kupitia ibada hiyo kwa kuacha anavyo vipenda, na kuyazuia mataminio yake. Anaidhibti nafsi yake kwa kumcha Allah na kumuogopa kila sehemu na kila wakati, katika siri na katika dhahiri. Kwa sababu hii, Allah Mtukufu anasema kuwa: «Enyi mlio amini, mmefaradhishiwa kufunga kama walivyofaradhishiwa waliokuwepo kabla yenu ili mpate kuwa wenye kumuogopa Allah». (Sura Albaqara, aya 183) Mazoezi ya kuacha maasi na madhambi Mwenye kufunga ajizuiapo kufanya mambo yaliyo halali kwa kufuata amri ya Allah atakuwa na uwezo zaidi wa kuyadhibiti mataminio yake ya kutaka kufanya maasi na madhambi, atachunga mipaka ya Allah na hatajiachia katika kufanya maovu. Mtume, swallalahu alayhi wasalam, amesema kuwa: «Mtu ambaye haachi kusema uzushi na kuufanyia kazi, basi Allah hana haja ya kuacha chakula chake na kinywaji chake». (Bukhari, Hadithi Na. 1804). Maana ni kwamba: Mtu ambaye haachi uongo na kufanya uchafu katika kauli na vitendo, huyo hajayafikia makusudio ya funga. Kuwakumbuka wenye shida na kuwasaidia Hiyo inatokana na kwamba katika funga kuna mazoezi ya kupambana na ukata, njaa, na kuwakumbuka maskini ambao wanapambana na hali ya kutokuwa na pato la kutosha siku zote. Kwa kufunga, mja huwakumbuka ndugu zake masikini na namna wanavyoteseka na mambo mawili machungu; njaa na kiu, na kwa sababu hiyo, atafanya juhudi ya kuwasaidia na kuwafariji.

UTUKUFU WA MJI WA MAKKA NA MSIKITI MTUKUFU