Kazi Za Wanawake KAtika UISLAM

Ni sahihi kwamba kutafuta na kupata kipato cha familia ni wajibu wa mwanaume na kwamba wanawake hawaruhusiwi na sheria ya Kiislamu kuwajibika kwa kitendo hiki. Hata hivyo, wanawake pia wanatakiwa kufanya kazi. Katika Uislamu kukaa bure ni fedheha na hukemewa.
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwenyezi Mungu Mweza wa yote anachukia kulala sana na kupumzika sana.”
Imam Sadiq (a.s) pia alisema: “Kulala sana hupoteza na kuharibu maisha ya mtu hapa duniani na Akhera.”
“Hadhrat Zahra (a.s) pia alikuwa akifanya kazi nyumbani”
Mtu yeyote mwenye kuhitaji na asiye hitaji, anatakiwa kuwa na kazi. Asipoteze bure maisha yake kwa kutofanya lolote, lakini anatakiwa kufanya kazi na kutoa mchango wake katika kujenga dunia iliyo bora.
Kama ni muhimu, mtu anatakiwa kutumia kipato chake kwa ajili ya familia yake na yeye mwenyewe, lakini kama kipato hicho hakihitajiki basi atoe msaada kwa wale wanao hitaji. Kukaa bure huchosha na mara nyingi husababisha maradhi ya kiakili na kisaikolojia na pia ufisadi.
Kazi iliyo bora zaidi kwa wanawake walioolewa ni kutunza nyumba. Utunzaji wa nyumba na watoto na kadhalika ni kazi nzuri na rahisi zaidi ambazo zinaweza kufanywa na wanawake.
Mwanamke aliyeolewa mwenye kipaji na bidii kwenye kazi anaweza kuibadili nyumba yake na kuwa mahali pa Pepo kwa watoto na mume wake; na hii ni kazi inayofaa na yenye thamani.
Mtume (s.a.w.w) alisema: “Jihadi ya mwanamke ni hapo ambapo humwangalia na kumtunza mume wake vema.”
Umm-e-Salamah alimuuliza Mtume (s.a.w.w.w): “Ni thawabu kiasi gani zimekadiriwa kwa kazi ya nyumbani kwa mke wa mtu?” Mtume (s.a.w.w) alijibu: “ Mwanamke yeyote ambaye anaipanga nyumba ionekane nadhifu, anachukua kitu fulani kutoka mahali fulani na kukiweka mahali pengine atafurahia neema za Mwenyezi Mungu, na mtu yeyote mwenye mvuto wa neema za Mwenyezi Mungu, hatateswa na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu.”
Umm-e-Salamah akasema: “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Wazazi wangu na watolewe muhanga kwa ajili yako, tafadhali taja thawabu zingine kwa ajili ya wanawake.” Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke anapokuwa mja mzito, Mwenyezi Mungu humpa yeye thawabu nyingi kama zile ambazo angepata mtu anayepigana vita vya Jihadi kwa kutumia utajiri wake na uhai wake. Halafu mwanamke anapojifungua mtoto wake, wito humfikia na kusema, ‘dhambi zake zote zimesamehewa; anza maisha mapya tena.’ Kila anapomnyonyesha mtoto wake maziwa yake, Mwenyezi Mungu humpa thawabu sawa na zile anazompa mtu anapomwacha huru mtumwa katika kipindi anacho mnyonyesha.”
Hata hivyo, hata wanapokuwa hawashughuliki na kazi za nyumbani, wanatakiwa kutafuta kitu cha kufanya, wanaweza kusoma vitabu, kufanya utafiti wa kitu chenye manufaa, ili wajiongezee ujuzi na kustadi wao. Wanaweza kuandika makala na hata vitabu. Wanaweza kuwa wachoraji, mafundi wa kupaka rangi, ufundi cherehani na kadhalika. Matokeo yake ni kwamba wanaweza kusaidia familia zao kiuchumi na pia kutoa mchango kwa jamii yao kwa kudhihirisha mafanikio yao kwa umma.
Kufanya kazi huzuia kuendelea kuwepo kwa maradhi ya akili.
Imam Ali (a.s) alisema: “Mwenyezi Mungu humpenda mchamungu ambaye kwa uaminifu anajishughulisha na kazi.”
Wakati ambapo baadhi ya wanawake hufanya kazi nyumbani, wapo wengine ambao hupenda kazi ya nje. Upendeleo huu ama unaweza kuwa kwa sababu ya kiuchumi au zingine. Kwa vyovyote vile, kazi nzuri kuliko zote ni zile za kitamaduni au uuguzi. Shule za vidudu, msingi, sekondari na sehemu zinazofaa kwa wanwake kufundisha na kuongoza wanafunzi wanawake. Mahospitali pia ni sehemu ambazo zinafaa kwa wanawake kutoa huduma ya uuguzi na udaktari.
Kazi kama hizi zinakubalika kwa maumbile ya kike; na pia mara chache sana, inapobidi wao kukutana na wanamume ambao si mahram (wanaume ambao sio ndugu wa karibu na ambao imeharamnishwa kufunga ndoa nao).
Yafuatayo ni mapendekezo kwa wanawake wenye nia au wanaofanya kazi nje ya nyumba zao:
Pata ushauri kutoka kwa mumeo kabla ya kuanza kufanya kazi. Ni haki ya mueo kukabali au kukataa kukupa ruhusa ya kufanya kazi. Kuanza kufanya kazi bila ruhusa ya mumeo inaweza kusababisha madhara kwenye mazingira tulivu ya kupendana katika familia yenu. Wanaume pia wanashauriwa kuwa wagumu kukubali wake zao kufanya kazi nje ya nyumba zao, isipokuwa kazi husika iwe haifai kwa wanamume.
Wanawake lazima wawe waangalifu kuhusu vazi la Hijabu ya kiislamu wanapokuwa nje ya nyumba zao. Lazima waende kazini bila kujipodoa na wavae nguo zisizo na urembo. Lazima waepuke kuchanganyika na wanaume ambao si mahram kwao kadiri iwezekanavyo. Ofisi ni mahali pa kazi si mahali pa kujionesha au mashindano.
Sifa njema na heshima ni sifa zisizoletwa na kivazi chako, lakini husababishwa na matendo yako, na matendo hayo unayafanua vema kiasi gani. Matendo yako yawe kama mwanamke wa kiislamu anaye heshimika. Dumisha tabia ya kujiheshimu mwenyewe, na usiziumize hisia za mume wako; mapambo yako na nguo zako nzuri sana, vaa unapokuwa nyumbani kwa ajili ya mume wako.
Wanawake wanatakiwa kuwa na tahadhari kwamba licha ya wao kufanya kazi nje ya nyumba zao, bado wanategemewa na waume zao na watoto wao kutoa huduma za shughuli, kama utunzaji wa nyumba, kupika, kufua na kadhalika.
Shughuli hizi zinaweza kufanywa kwa ushirikiano wa kifamilia. Kazi ya nje ya nyumba isiwe sababu ya kuitibua familia yote. Wanaume pia wanashauriwa kuwasaidia wake zao kuhusu utunzaji wa nyumba. Waume wasiwategemee wake zao kufanya kazi nje na nyumbani pake yao. Matumaini ya aina hii wala si halali ama haki. Wanaume na wanawake lazima wagawane kazi za nyumbani.
Kama mwanamke, ambaye anafanya kazi nje ya nyumba anaye mtoto, basi anatakiwa amwache mtoto kwenye shule ya chekechea au mtu anayeaminika na mwema. Wala si haki au busara kuwaacha watoto nyumbani bila mtu wa kuwatunza, kwani watoto wengi huwa waoga au kujihisi hawana msaada wanapo kabiliana na hali ya hatari.
Kama mwanamke anahisi kwamba, zaidi ya kazi zilizotajwa hapo juu na wajibu uliotajwa hapo juu, lazima afanye kazi nyingine, basi ni lazima aelewane na mume wake wazi wazi na aanze kufanya kazi hiyo kwa ruhusa yake na ushauri wake. Kama mume atakataa, mke lazima aache mpango huu. Kama mume atakubali mke wake afanye kazi, lazima achague kazi ambayo itamkutanisha na wageni wanaume wachache sana. Hii ni kwa manufaa yake na jamii. Kwa vyovyote vile, anapokuwa nje ya nyumba yake, lazima awe makini kufuata kanuni za vazi la kiislamu la Hijabu na asijipodoe kabisa.

Usipoteze Muda Wako Wa Akiba

Kazi za nyumbani huwa za aina nyingi mbali mbali. Kama mke anayo nia ya kufanya kazi kwa ubora zaidi hatoweza kuwa na muda wa kutosha wa kufanya kitu kingine. Huu ni ukweli hususan ambapo pia mama wa nyumbani anatakiwa kuwatunza watoto. Lakini wanawake walio wengi ambao wameolewa hupata muda wa akiba.
Kila mtu hutumia muda wake wa akiba kwa njia moja au nyingine. Wanawake wengine hupoteza muda wao wa akiba. Wanaweza tu kutembea mtaani au anazungumza na mwanamke mwingine. Mara nyingi mazungumzo yao ya saa chache hayana thamani yoyote. Wanaweza kusikiliza maneno ya kurudia rudia ambayo huthibitisha ni ya kupoteza muda na fadhaa.
Porojo za bure kama hizo husababisha kuvunjika heshima na maadili. Wanawake wanaopitia maisha ya namna hii, hakika wanapata hasara katika dunia hii na ile ijayo. Ni ajabu ilioje kwamba kama mtu yeyote anapoteza fedha, anatibuka sana, lakini watu hawafikirii hata kidogo kuhusu kupoteza muda wao wenye thamani katika maisha yao.
Mtu mwenye busara hujitahidi sana kutumia saa zenye thamani za maisha yake kwa manufaa. Ni mafanikio ya thamani kiasi gani mtu anaweza kuwa nayo!
Uvivu una madhara na husababisha maradhi ya akili na kuchanganyikiwa. Mtu mvivu wakati wote huwa katika mawazo na hutafuta njia za kuhisi huzuni.
Hupata aina nyingi za wasi wasi na baadaye akili yake huvurugika. Mtu mwenye furaha ni yule ambaye wakati wote anashughulika kufanya kitu fulani. Mtu mwenye bahati mbaya ni yule ambaye ni mvivu sana na hutumia muda wa ziada wa kutosha kufikiri raha na taabu za maisha yake. Kujishughulisha ni jambo la kufurahisha na uzembe ni chanzo cha mfadhaiko.
Je, si jambo la kusikitisha kwamba mtu anaweza kupoteza maisha yake yenye thamani au kutumia kiasi cha muda wake bila kunufaika kwa namna yoyote?
Bibi mpendwa! Unaweza kutumia kwa manufaa makubwa muda wako wa akiba. Unaweza kufanya kazi za kisayansi. Unaweza kununua vitabu vinavyo husiana na taaluma hiyo na kwa msaada wa mume wako, utaongeza ujuzi. Masomo ya kozi yoyote inawezekana, fizikia, kemia, Qur’ani, falsafa, historia, fasihi, saikolojia na kadhalika. Ungefurahia muda huo na labda siku moja ungetoa mchango wako kwa jamii kwa ujuzi wako. Unaweza kuandika makala au hata vitabu ambapo baadaye jina lako litaendelea kudumu. Pia unaweza kujipatia fedha.
Usidhani ya kwamba wanawake wote mashuhuri katika historia wanakuwa wakizembea. Wao pia waliolewa lakini ni hao ambao hawakupoteza bure muda wao wa akiba.
Bibi Dorothy Carnegie, alikuwa ameolewa na ambaye aliandika kitabu kizuri. Alikuwa akifanya kazi za nyumbani na pia alimsaidia mume wake (Dale Carnegie) kuandika kitabu chake maarufu; “How to make friends and Infuluence People.” Ameandika kwenye kitabu chake kuhusu kanuni za kumtunza mume: “Nimeandika kitabu hiki wakati mwanangu anapolala kwa muda wa saa mbili. Nilikuwa nasoma sana wakati ambapo nywele zangu zilikuwa zinakaushwa kwenye chumba cha kutengeneza nywele.”
Wapo wanawake wengi ambao wameandika vitabu maarufu wanapata mafanikio mengi katika uwanja wa sayansi.
Kama wewe ni mtu mwenye shauku, ungekuwa mmojawao. Kama mume wako ni mtafiti basi msaidie katika taaluma yake. Je, si jambo la kusikitisha kwa mwanamke msomi kutokutumia ujuzi wake wote?
Imamu Ali (a.s) alisema: “Hakuna hazina iliyo bora zaidi ya ujuzi.”
Imamu Baqir (a.s) alisema: “Yeyote anayetumia mchana na usiku kwa kutafuta ujuzi, kwa hakika ataunganishwa na neema za Mwenyzi Mungu.”
Kama wewe hupendelei kusoma au kutafiti basi jishughulishe na kazi za mkono au uchoraji kama kushona nguo, kupaka rangi, kufuma, mapambo ya maua, na kadhalika.
Unaweza kujifunza sanaa za aina hii na kuzifanyia mazoezi. Itikadi hizi zinaweza kukusaidia kiakili na kiuchumi. Uislamu pia umependekeza kazi za mikono zifanywe na wanawake wakati wa muda wao wa akiba. “Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alisema: “Kusokota na kufuma ni burudani nzuri kwa wanawake.”

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KUSWALI HATUA KWA HATUA

UTUKUFU WA MJI WA MAKKA NA MSIKITI MTUKUFU

Kisa Cha Nabii Ibraahiym عليه السلام - Sehemu Ya 1