Heshima Ya Mume

Hamu ya kuheshimiwa ni jambo la asili, lakini si kila mtu yupo tayari kuitoa. Mumeo
hukutana na watu wengi katika shughuli zake wakati hayupo nyumbani. Baadhi ya watu hao wanaweza kuwa hawana staha na kumfedhehesha hali ambayo hatimaye humtibua mtu.
Wewe kama mke wake, anakutarajia wewe kuonesha heshima na ari akiwa nyumbani na kwa hali hiyo unaipandisha hadhi ya nafsi yake iliyokanyagwa.
Kumstahi na kumheshimu mume wako hakukudhalilishi wewe, lakini huongeza nguvu na mwelekeo kwenye harakati za kuyafanya maisha kuwa bora. Kila mara unatakiwa umsalimie na kwa hayo maamkizi yako mfanye ahisi unamjali. Usiingilie kati mazungumzo yake. Uwe na adabu na mpole unapozungumza naye na usimpigie makelele. Inapotokea wote wawili mnakwenda kwenye mkutano ngoja mumeo aingie kwanza. Msifie mbele ya watu wengine. Waambie watoto wenu kumheshimu baba yao na uwakaripie kama hawaoneshi adabu kwake. Mheshimu mbele ya wageni na uwe makini kwa mahitaji yake, na yale ya wageni.
Anapogonga mlango jaribu kufungua mlango huku ukitabasamu na kuonesha uso wenye furaha. Tendo hili dogo la kuonesha furaha, athari yake ni kwamba huburudisha moyo na kumwondolea uchovu mumeo. Baadhi ya wanawake wanaweza kudhani kwamba tabia ya aina hiyo si ya kawaida. Fikiria unapomwamkia mumeo kama mgeni. Hii si tabia nzuri kwa sababu mumeo amekuwa kwenye harakati siku nzima kwa ajili ya ustawi wa familia yake na anastahiki kufikiriwa na kuheshimiwa anaporudi nyumbani. Maamkuzi hayo ya kwanza huleta picha nzuri sana, na lililo zuri kwa mgeni ni zuri pia kwa jamaa wa familia.
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Wajibu wa mwanamke ni kujibu hodi ya mlangoni na kumkaribisha mume wake.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwanamke anayemheshimu mume wake na hamsumbui, atapata bahati na mafanikio.”
Mtukufu Mtume (s.a.w) alisema: “Mke anawajibika kutayarisha beseni na taulo ili mumewe anawe mikono.”
Uwe mwangalifu usije ukamfedhehesha mumeo, usizungumze naye kwa ukali, usimtukane, uwe msikivu kwake na usimuite kwa majina machafu. Ukimkosea na yeye atakufedhehesha wewe. Hatimaye, moyo wa mapenzi na kuaminiana utamomonyoka. Kwa hiyo, mtagombana mara kwa mara na kubishana, hali ambayo itasababisha mtalikiane.
Hata kama mtaendelea kuishi pamoja, maisha yenu kwa hakika yatajaa fujo. Hisia za uadui na usumbufu wa kisaikolojia unaweza kuanza kujengeka hadi kufikia kiwango cha kuhatarisha maisha ya wanandoa na hali hiyo inaweza kusababisha uhalifu. visa vifuatavyo vinaonesha baadhi ya mambo haya:
“Mtu mmoja mwenye umri wa miaka ishirini alimchoma kisu mkewe mwenye umri wa miaka kumi na tisa hadi akafa kwa sababu mke alimtukana mume. Mahakamani mume alisema; ‘nilimuoa mwanamke huyu mwaka moja uliopita. Mwanzoni mke wangu alinipenda sana. Lakini baada ya kipindi kifupi mke wangu alibadilika na kuanza kunidhalilisha.
Alianza kutumia lugha ya matusi kwangu kila ilipowezekana na kwa sababu ndogo sana, alianza kunikebehi. Kwa sababu jicho langu la kushoto ni kengeza, akawa na desturi ya kuniita mimi ‘punda kipofu.’ Siku moja, akaniita ‘punda kipofu’ nilikasirika sana hivyo kwamba nilimchoma kisu mara kumi na tano.’ ”
“Mtu mwenye umri wa miaka sabini na moja (71) ambaye alimuua mkewe, alitoa maelezo yafuatayo: ‘Ghafla tabia ilibadilika kwangu na akaanza kutonijali mimi. Wakati mmoja akaniita ‘mtu nisiyevumilika.’ nikagundua kwamba alikuwa hanipendi tena, nikamshuku na nilimuua kwa kumkata shoka mara mbili.”

Malalamiko Na Manung’uniko

Hakuna mtu yeyote asiyekuwa na matatizo na manung’uniko kuhusiana na maisha ya kila siku. Kila mtu hupenda kuwa na mtu wa kumhurumia ambaye anaweza kuwa mwandani wake na kumsikiliza matatizo yake. Lakini jambo la kukumbuka ni kwamba “upo wakati na mahali kwa kila jambo.” Mtu lazima aelewe wakati muafaka na mahali pa kulalamikia. Baadhi ya wanawake wajinga na wabinafsi hawatambui kwamba waume zao wanachoka sana na fadhaa baada ya kazi ya siku nzima. Badala ya kungoja kwa muda wa saa moja au mbili ili apumzike na kupata nguvu, huanza kumshambulia kwa mfululizo wa malalamiko. Mathalani mke anaweza kusema:
“uliniacha mimi na watoto hawa maluuni na ukaenda zako. Ahmad amevunja kioo cha mlango wa chumba cha mbele. Watoto wetu wa kike walipigana. Makelele ya watoto wa majirani zetu yananiudhi kweli. Hasan hajifunzi hata kidogo na amepata maksi za chini sana. Nimefanya kazi sana leo najisikia nimechoka. Hakuna hata mtu wa kusikiliza kilio changu!
“Watoto hawa hawanisaidii hata kidogo kwa kazi za hapa ndani. Afadhali nisingezaa watoto kabisa! Unayo habari dada yako alikuwa hapa leo? Sijui tatizo lake nini; alikuwa anafanya mambo kama vile nimemeza urithi wa baba yake.
“Mungu na aninusuru kutoka na mama yako! Amekuwa ananisengenya. Nimechoshwa na wote hao. Pia nimejikata kidole leo kwa kisu na kuumia sana.
“Ingekuwa vema kama nisingekwenda kwenye harusi ya Muhamedi jana. Ungemuona mke wa Rashid! Alivyopendeza, ungeshangaa! Mwenyezi Mungu angenipa na mimi bahati kama hiyo! Wanaume wengine wanawapenda wake zao na huwanunulia vitu vizuri. Hao ndio waoaji wa kweli.
“Rashid alipoingia kila mtu alimpa heshima. Ni kweli kwamba watu hupendelea kuona tu vazi ulilovaa. Anacho nini ambacho mimi sina? Kwa nini ajioneshe mbele yangu? Ndio, anayo bahati kuolewa na mume ambaye anampenda, yeye si kama wewe!
“Siwezi kuvumilia kuendelea kuishi kwenye nyumba iliyolaaniwa, kukutunza wewe na watoto. Kwa hiyo fanya utakalo!”
Msimamo wa namna hi si sahihi. Wanawake wa aina hii hudhani kwamba waume zao huondoka kwenda kwenye pikiniki au burudani kila asubuhi. Wanaume hukutana na mamia ya matatizo kila siku. Bibi mpenzi! Hujui mumeo amepita kwenye mambo gani anapokuwa katika kazi yake. Hujui ni watu fidhuli na wenye karaha kiwango gani mumeo ameshughulika nao siku nzima. Kwa hiyo, anapokuja nyumbani usiwasilishe malalamiko yako yote kwa wakati moja. Usimfanye ajihisi kuwa imekuwa hatia kuwa mwanamume.
Uwe na wastani na umfikirie. Endapo kwa kunung’unika kwako na kumsumbua, kutamuongezea wasi wasi na machungu, basi, ama anaweza akaanza ugomvi au akaondoka hapo nyumbani na kwenda kwenye mgahawa au filamu au hata kutembea tu mitaani.
Kwa hiyo, ewe Bibi mpenzi! Kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, acha mazoea haya ya kulalamika hata wakati usio muafaka. Tafuta muda unaofaa na halafu mpe matatizo yako ambayo ni ya kweli, si kwa kulalamika, lakini fanya hivyo, kwa namna ya kushauriana. Kwa njia hii, hutasababisha yeye kuanza kujenga hisia za uadui na mapatano ya familia yanabaki kuwa salama.
Mtume (s.a.w.w) wa Uislamu alisema:
“Sala za mwanamke anayemchokoza mume wake kwa ulimi wake, hazikubaliwi na Mwenyezi Mungu hata kama akifunga saumu kila siku, anaamka kila siku usiku kufanya ibada, anawaachia huru watumwa katika njia ya Mwenyezi Mungu. Mwanamke mwenye ulimi mbaya ambaye humuumiza mumewe kwa njia hii, ni mtu wa kwanza kuingia Jahanamu!”
Mtukufu Mtume (s.a.w.w) pia alisema: “Wanawake wa Peponi huwaambia wanawake wanaowatukana waume zao kwa njia hii: ‘Mwenyezi Mungu na akuuweni. Msiwe watovu wa adabu kwa waume zenu. Mtu huyu (mume) si kiumbe wako, na wewe hustahiki kuwa naye. Muda mfupi ujao atakuacha na atakuja kwetu.’ ”
Sijui wanawake wa aina hii wanataka kujipatia nini kwa hayo manung’uniko yao. Kama wanataka kusikilizwa na waume zao au kujionesha, basi, hakika wanajipatia kitu kinyume chake kabisa na kumkasirisha. Kama wanakusudia mateso kwa mume, kumsababishia madhara ya kisaikolojia na kumuingiza kwenye mazoea bandia ya kuangamiza, basi wapo kwenye njia potofu.
Bibi mpendwa! Kama unamjali mumeo na familia yako, basi ni lazima uache msimamo huu usio na mantiki. Je, umewahi hata kufikiria kwamba mwenendo wako mbaya unaweza ukasababisha kuvunjika kwa maisha ya familia yako?
“Daktari mmoja alitoa ushahidi mahakamani: ‘Sijapata kumuona mke wangu akifanya mambo kama mke sahihi wa nyumbani wakati wote wa ndoa yetu. Nyumba yetu mara nyingi imekuwa katika machafuko.Wakati wote mke wangu anapiga makelele na kutukana. Nimechoshwa naye.’ Baada ya kumlipa mke wake fedha nyingi tu, akapata talaka. Akasema kwa furaha: ‘Kama angetaka na angeomba utajiri wangu wote na hata shahada yangu ya taaluma ya tiba, ningempa ili niachane naye haraka sana.’ ”

Tabia Za Kupendeza

Mtu yeyote mwenye tabia njema na inayopendeza pia angepata dhiki na matatizo ya maisha kwa njia ile ile. Hawa ni aina ya watu ambao watu huvutiwa nao na wanawatafuta wakati wote. Tabia inayopendeza na msimamo wa mtu utakuwa na kinga dhidi ya maradhi ya kisaikolojia kwa kuwa kuonekana kwao katika maisha ni kushinda matatizo yao kwa njia nzuri iwezekanayo.
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Hakuna maisha yanayo kubalika zaidi kuliko yale ambayo yanatokana na tabia njema.”
Lakini mtu mwenye tabia mbaya naye pia angeyaona maisha hayafurahishi kwani uhusiano wa watu hao kuendeleza wasiwasi na fadhaa.
Mtu kama huyu hupenda kulalamika na kupigia kelele maisha. Msimamo wa namna hii huepukwa na watu wengi ambapo mtu huyo hapati marafiki wengi. Hii ndio hali ambayo huathirika kwa urahisi na matatizo mbali mbali ya kisaikolojia na maradhi mengineyo kwa sababu ya wasi wasi na utupu ambao mtu mwenye msimamo mbaya anavyoyaona maisha.
Mtukufu Mtume (s.a.s) alisema: “Mtu mwenye tabia na msimamo mbaya atakuwa kwenye masumbuko na mateso wakati wote.”
Msimamo mzuri na unaopendeza ni muhimu kwa watu wote kwa ujumla na hususan baina ya wanandoa kwani wanandoa lazima wawe pamoja.
Mpendwa Bibi! Kama unataka kufurahia maisha ya furaha na mumeo na watoto wako, ufanye msimamo wako na tabia ya kupendeza vikubalike. Uwe na tabia njema na si mgomvi. Unao uwezo wa kuifanya nyumba yako kuwa Pepo ya hali ya juu au Jahanamu iwakayo moto. Unaweza kuwa malaika wa huruma ambapo mumeo na watoto wanaweza kupata amani kupitia kwako.
Unajua utaacha mvuto wa kupendeza kiasi kwenye roho zao kwa huo msimamo wako wa kutabasamu na lugha nzuri.
Mvuto wa kupendeza ni mbichi katika akili zao wanapoondoka kwenda shuleni au kwenye shughuli za kazi na unawasaidia wao kuwa na mwanzo mzuri wa siku.
Kwa hiyo, kama unajali kuhusu sifa nzuri ya maisha yako na uhusiano ulio nao na mumeo, usiwe kinyume na tabia njema. Uwe dhahiri katika msimamo wako na tabia inayopendeza kwani nguzo bora zaidi ya kutegemea kwa usalama wa ndoa ni maadili mazuri ambayo yanaelekeza kwenye tabia inayopendeza.
Namna nyingi za talaka ni kwa sababu ya tabia zisizolingana za mume na mke. Takwimu juu ya talaka kwa uthibitisho zinaonesha kwamba msimamo wa kupatana, maadili mema na tabia ya kupendeza, hazikuwepo kwa wanandoa husika. Chanzo kikubwa cha ugomvi na kutokuelewana kwa wanandoa ni kwa sababu yakutolingana kwa tabia na kanuni za maadili za wanandoa. Takwimu zifuatazo zinavutia:
“Mwaka 1968 kesi za malalamiko ya ndoa zilizowasilishwa mahakamani zilikuwa 16,039, kesi 12,760 miongoni mwa hizo, misingi ya malalamiko yao ilikuwa kutokulingana kwa kanuni za maadili. Mwaka 1969 kesi za malalamiko ya aina hiyo hiyo 16,058 liziwasilishwa mahakamani, kesi 11,246 miongoni mwa kesi hizo, misingi ya malalamiko ilifanana na ile ya kesi za mwaka wa nyuma. Kwa hiyo, inathibitika kwamba zaidi ya asilimia sabini ya ugomvi wa kifamilia ulisababishwa na kipengele hiki.”
Mwanamke alilalamika kwenye Baraza kwamba mume wake kila siku alikuwa na desturi ya kula chakula chake cha mchana na jioni nje.
Halafu mwanaume akaeleza kwamba sababu iliyomfanya ale nje ni kwamba mke wake hakuwa mbunifu hata kidogo na alikuwa mwenye tabia isiyopendeza kuliko wanawake wote wenye tabia kama hiyo hapa duniani. Haraka sana mwanamke alinyanyuka na kuanza kumpiga mume wake mbele ya majaji.”
Mwanamke huyu mpumbavu alidhani kwamba angebadilisha tabia ya mume wake ya kula chakula chake nje badala ya nyumbani kwa kulalamika, kutukana na kumpiga.
Lakini mwanamke huyu hakutumia mbinu rahisi na ya kiakili ambapo alitakiwa kuwa na busara zaidi na kuzingatia mwenendo unaostahili.
Mwanamke mwingine alipeleka taarifa mahakamani kwamba mume wake aliacha kusema naye kwa muda wa miezi 15 na kwamba alikuwa anatoa matumizi yake kupitia kwa mama yake (mume). Mume alijibu kwamba alikwisha kinai na msimamo usiopendeza wa mke wake ambao ulimfanya yeye asizungumze naye kwa miezi.”15
Migongano mingi ya kifamilia inaweza kusuluhishwa kwa wema, huruma na tabia inayopendeza. Kama mume wako si mwema, kama anatoka kwenda kula chakula cha jioni peke yake, kama anapenda kutumia lugha ya matusi, anatumia utajiri wake wote vibaya, hupenda kusema suala la kutalikiana na kutengana au sababu kadhaa katika ugomvi wa kifamilia, ipo njia moja tu ya kusuluhisha. Njia hii ni kuwa mwema na tabia njema. Matokeo ya mazoea ya tabia kama hii ni ya kimiujiza.
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwenyezi Mungu Mweza wa yote atampa mtu mwenye tabia ya kupendeza thawabu zinazolingana na zile za Jihadi. Atamneemesha kwa wingi mtu huyo usiku na mchana.”
Imam Sadiq (a.s) alisema: “Mwanamke yeyote anaye msumbua na kumtesa mumewe yu mbali na neema za Mwenyezi Mungu na mwanamke yeyote anayemheshimu, anaye mtii na hamhuzunishi mumewe, ameneemeka na kufanikiwa.”
Ipo hadith inayosema kwamba Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alipewa taarifa ya mwanamke mwema ambaye alifunga saumu kila siku na alikuwa anafanya ibada kila siku usiku akimuabudu Mwenyezi Mungu, lakini alikuwa na tabia isiyo pendeza ya kuwaudhi majirani zake kwa maneno yake makali. Mtukufu Mtume alisema: “Hapana jema kwake huyo na yeye ni mkazi wa Jahanamu.”

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KUSWALI HATUA KWA HATUA

UTUKUFU WA MJI WA MAKKA NA MSIKITI MTUKUFU

Kisa Cha Nabii Ibraahiym عليه السلام - Sehemu Ya 1